Queen Darleen afunguka maisha na mke mwenzie

Muktasari:

Queen Darleen aliolewa mke wa pili na mwanaume anayeitwa Ishaq Mtoro, Desemba, 2019 ambapo imekuwa kati ya ndoa za mastaa zinazofuatiliwa kwa sasa hapa nchini

MSANII wa Bongo Fleva kutoka lebo ya WCB, Queen Darleen, ameeleza maisha wanayoishi yeye na mke mwenzie tangu alipoolewa.

Queen Darleen ambaye jina lake halisi ni Mwanahawa Abdul, aliolewa mke wa pili  na mwanaume anayeitwa Ishaq Mtoro, Desemba, 2019 ambapo imekuwa kati ya ndoa za mastaa zinazofuatiliwa kwa sasa nchini.

Katika mahojiano na kituo cha Televisheni cha Wasafi, pamoja na mambo mengine aliweka bayana namna wanavyoishi na mke mwenzake anayejulikana kwa jina la Sabra, ambaye baadhi ya watu wameonekana kumtuhumu mumuwe kuwa anampendelea kwa kuwanaye muda mwingi.

Akilizungumzia hili, msanii huyo amesema ukweli ni kwamba tofauti na watu wanavyodhani  ni kwamba Ishaq analala siku nne kwa mke mkubwa na kwake huwa akilala siku tatu.

“Huwezi amini mume wangu kwangu analala siku tatu, lakini ukweli ni kwamba ni mtu unayemuona akiwa kwangu anafurahi sana, sijisifii na unaweza kutafuta muda umuulize mwenyewe.

“Pia hata siku ambayo ana zamu ya kulala kwa mwenzangu ni lazima tuonane naye na hii ni kutokana na kufanya kazi ambazo zinafanana kwani yeye ofisini kwao wana studio, hivyo huwa akinipitia tunaenda naye huko,” amesema  Queen ambaye ni dada wa msanii Diamond Platnumz .

Ameongeza kuwa huwa  anapomuweka kwenye mitandao akiwa naye sio kwamba saa zote yupo naye, sema amempa uhuru wa kufanya hivyo wakati wowote anapojisikia.

Katika hili amesema akiwa kama msanii anafanya hivyo kwa lengo la kuifundisha jamii kwani kuna wanawake wengine wakiolewa wanajisahahu na kuona kama wamemaliza kila kitu,bila kujua mwanaume anapaswa kulelewa.