Niyonzima, Chama waipeleka Simba robo fainali

Muktasari:

Kipindi cha pili Simba walibadilika kwa kushambulia zaidi hasa baada ya kufanya mabadiliko katika eneo la kiungo ambalo walionekana kukamatwa katika kipindi cha kwanza.

 KLABU ya Simba imefanikiwa kutinga hatua ya robo fainali baada ya kuichapa 2-1 AS Vita katika Uwanja wa Taifa.

 Simba wamefikisha pointi 9 huku  Al Ahly wakifikisha alama  10 baada ya kuifunga JS Saoura mabao 3-0 leo.

Katika mchezo huo As Vital walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Francy Kasengu lakini Simba walichomoa kupitia kwa Mohammed Hussein na mpira kwenda mapumziko wakiwa 1-1.

Kipindi cha pili Simba walibadilika kwa kushambulia zaidi hasa baada ya kufanya mabadiliko katika eneo la kiungo ambalo walionekana kukamatwa katika kipindi cha kwanza.

Dakika 54 Simba walishambulia kupitia upande wa kushoto baada ya Emmanuel Okwi kutumia spidi na kugongeana na John Bocco aliyepiga pasi fupi hata hivyo Kagere alishindwa kuumalizia mpira huo licha ya kubaki yeye na nyavu.

Dakika 57 Simba walifanya mabadiliko kwa kumtoa Emmanuel Okwi na kuingia Haruna Niyonzima, mabadiliko hayo yalionyesha kutaka kuongeza nguvu kwenye eneo la kiungo. Niyonzima alianza kuonyesha makeke yake mapema tu baada ya dakika 59 kupiga pasi mpenyezo kwa John Bocco ambaye alipiga pasi ya ndani hata hivyo umakini kwa Kagere ulipungua.

As vita walifanya mabadiliko dakika 60 kwa kumtoa Tuisia kisinda na kuingia Ducapel Moloko na dakika 63 walimtoa Mundele Makusu na kuingia Manzoki Lobi. Makusu katika mchezo huu alishindwa kabisa kuonyesha makeke yake ambayo amezoeleka baada ya kuwa chini ya ulinzi wa Pascal Wawa, lakini alikuwa na utulivu katika kukaa na mpira tofauti na Manzoki Lobi aliyechukua nafasi yake.

Dakika 71 AS Vita walifanya mabadiliko mengine kwa kuingia Mumbere Mussa na kumtoa Bopunga Botuli. Simba walionekana kutawala mpira zaidi tangu alipoingia Haruna Niyonzima, lakini kocha Patrick Aussems alifanya mabadiliko mengine dakika 77 kwa kumuingiza Hassan Dilunga aliyechukua nafasi ya Mzamiru Yassin. Dakika 83 Kagere alipenyezewa pasi na Haruna Niyonzima akiwa ndani ya dimba.