Gor Mahia, KCCA zakomaa, Yanga, Bandari majanga tupu

Muktasari:

Katika michezo hiyo ya hatua ya mtoano iliyofanyika mwishoni mwa wiki ilishuhudia timu mbili zikifungwa na nyingine tatu zikitoka sare..

Dar es Salaam.Matumaini ya Afrika Mashariki kuwa na timu nyingi katika hatua ya Kombe la Shirikisho Afrika yameingia doa baada ya klabu zake Yanga, Gor Mahia, KCCA, Bandari na Proline kupata matokeo mabaya.

Katika michezo hiyo ya hatua ya mtoano iliyofanyika mwishoni mwa wiki ilishuhudia timu mbili zikifungwa na nyingine tatu zikitoka sare.

Miamba ya Tanzania, Yanga ilikubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Pyramids katika mchezo uliochezwa kwenye Uwanja wa Kirumba, Mwanza.

Wageni Pyramids walipata mabao yao mawili yaliyofungwa na El Said na Traore wakati lile la Yanga lilifungwa na Papy Tshibimbi.

Yanga inahitaji muujiza katika mchezo wake wa marudiano utakaofanyika siku saba zijazo ili kufuzu kwa hatua ya makundi.

Mabingwa wa Kenya, Gor Mahia ililazimishwa sare 1-1 nyumbani na Motema Pembe ya DR Congo sasa wanahitaji suluhu au ushindi ili kufuzu kwa hatua ya makundi.

Bandari ya Kenya ikiwa ugenini ilikubali kipigo cha mabao 4-2 kutoka kwa Horoya ya Guinea, sasa watalazimika kutumia vizuri uwanja wa nyumbani wiki ijayo ili kurudisha matumaini ya yao ya kusonga mbele.

Mshambuliaji wa Burkina Faso, Aristide Bance alifunga mabao matatu ‘hat-trick’ na Ocansey Mandela alifunga bao kwa Horoya, huku Abdallah Hassan akifunga mabao mawili kwa Bandari FC katika mchezo huo uliofanyika Conakry.

Mabingwa wa Uganda, KCCA ikiwa nyumbani ililazishwa suluhu na Paradou ya Algeria katika mchezo uliochezwa Lugogo.

Proline mara mbili ilitoka nyuma katika sare ya mabao 2-2 dhidi ya Al Nasr ya Libya katika mchezo wa kwanza wa mtoano uliofanyika Misri.

Bright Anukani na Mustafa Mujjuzi walifunga mabao ya kusawazisha ya Proline dhidi ya Al Nasr.

Waganda hao sasa wanahitaji suluhu au sare 1-1 katika mchezo wa marudiano jijini Kampala kusonga mbele wakati Al Nasr ni lazima washinde au wapate sare ya zaidi ya mabao matatu ili kusonga mbele.

Katika michezo mingine Fosa Juniors ya Madagascar imewaduwaza RS Berkene ya Morocco kwa kuichapa mabao 2-0.

Miamba ya Afrika Kusini, Bidvest Wits imeshinda 2-1 ugenini dhidi ya UD Songo ya Msumbiji, Green Eagles ya Zambia ililazimishwa sare 1-1 na Hassania Agadir ya Morocco huku El Masry ikishinda ushindi mnono wa mabao 4-0 ugenini dhidi ya Cote d’Or ya Seychelles.

Matokeo

Yanga (Tanzania) 1-2 Pyramids (Misri)

Horoya (Guinea) 4-2 Bandari (Kenya)

Gor Mahia (Kenya) 1-1 Motema Pembe (DR Congo)

KCCA (Uganda) 0-0 Paradou (Algeria)

El Nasr (Libya) 2-2 Proline (Uganda)

Enyimba (Nigeria) 2-0 TS Galaxy (Afrika Kusini)

Kotoko (Ghana) 0-0 San Pedro (Ivory Coast)

UD Songo (Msumbiji) 1-2 Bidvest Wits (Afrika Kusini)

Elect Sport (Chad) 0-1 Djoliba (Bamako)

Green Eagles (Zambia) 1-1 HUSA (Morocco)

Cano Sport (Equatorial Guinea) 1-3 Zanaco (Zambia)

Fosa Juniors (Madagascar) 2-0 RS Berkane (Morocco)

Cote d’Or (Seychelles) 0-4 El Masry (Misri)

ASC Kara (Togo) 2-1 Rangers (Nigeria)

Nouadhibou (Mauritania) 2-0 Triangle (Zimbabwe)