Mashabiki Aston Villa wamtaka Samatta acheze dhidi ya Watford

Muktasari:

Samatta amesaini mkataba wa miaka minne na nusu kuichezea Aston Villa inayopambana na janga la kushuka daraja.

Dodoma. Mashabiki wa Aston Villa wameshindwa kuzuia hisia zao baada ya kumtaka kocha wao amtumie mshambuliaji wao mpya Mbwana Samatta aliyesaini mkataba wa miaka minne na nusu katika mchezo wa leo dhidi ya Watford.

Usiku wa kuamkia leo Aston Villa ilitangaza kukata kiu ya mashabiki wa timu hiyo kusajili mshambuliaji kufuatia kuumia kwa Wesley Moraes atakayekosekana kkwa msimu mzima uliobaki.

Pamoja na Samatta kumtangaza jana usiku ananafasi ndogo ya kuanza katika mchezo wa leo wa Ligi Kuu dhidi ya Watford.

Kupitia mitandao tofauti ya kijamii na zaidi mtandao maarufu wa mashabiki wa timu hiyo unaoitwa Villareport (twitter) ambao umetumiwa na mashabiki wa timu hiyo kushinikiza uwepo wa mshambuliaji (Samatta) katika mchezo huo.

Kibembe kilianzia kwa taarifa iliyowekwa na mwandishi Rob Dorsett aliyekuwepo katika mkutano wa meneja wa timu hiyo Dean Smith baada ya kuweka wazi kuwa Samatta hatawakabili Watford leo Jumanne.

Baada ya mwandishi huyo kuweka taarifa hiyo akihoji "inawezekana Aston Villa kuifunga Watford bila mshambuliaji?", akiweka katika mtindo wa swali ndio au hapana, kilichofuata ni malalamiko na masikitiko kwa mashabiki wengi waliotoa maoni yao wakionyesha wazi kutofurahia jambo hilo wakihitaji timu yao iwe na mshambuliaji kwenye mchezo wa leo.

Samatta ana uhakika wa kujumuishwa kwenye mchezo wa Januari 28 wa nusu fainali Kombe la Ligi dhidi ya Leicester City ukifuatiwa na ule wa Ligi Kuu dhidi ya Bournemouth Jumamosi Februari mosi.