Liverpool yapata pigo la pili baada ya kipigo 4-0

Muktasari:

  • Liverpool  imekumbana na kipigo cha pili kikubwa katika Ligi Kuu England wakiwa chini ya Jürgen Klopp vyote wamekumbana navyo wakiwa Etihad dhidi ya Manchester City (4-0 Jana na  5-0,  Septemba 2017).

London, England. Kocha wa Liverpool, Jurgen Klopp amewatetea wachezaji wake kwa kusema kipigo cha mabao 4-0 walichokipata kutoka kwa Manchester City hakijasababishwa na kubweteka kwao.
Matokeo hayo ni miongoni mwa vipigo vikubwa ambavyo timu iliyochukua ubingwa imekumbana navyo.
Klopp  alisema sio kweli kwamba kufungwa kwao kumetokana na kubweteka kwa wachezaji wake baada ya siku chache zilizopita kusheherekea ubingwa wa Ligi Kuu England.
"Niliona mapigano. Hatukuwa kama mtu ambaye amechukua ubingwa wiki iliyopita, kuna muda mchezo ulikuwa 50-50 lakini muda mwingine tulionekana kuwa wazito.
Walitumia nafasi ambazo walipata kwetu haikuwa hivyo, walikuwa bora kwa  asilimia 100 walistahili, lakini iliwezekana matokeo kuwa 5-5. Lakini matokeo yakawa ya 4-0 na tunapaswa kupata somo hapo," alisema Klopp
Klopp alisema kuwa timu yake iliupa uzito mkubwa mechi hiyo na ilikuwa na uwezekano wa kupata ushindi.
 "Ninapenda timu yangu jinsi walivyouanza mchezo. Nilisema hivyo na nilidhani hiyo ilikuwa wazi. Nadhani hiyo ni wazi. tulithibitisha hatua hiyo. Na City wamethibitisha kuwa wao ni timu nzuri," alisema Klopp.