Huyu jamaa anaitaka jezi ya Morrison Yanga

Kiungo mshambuliaji wa Alliance, David Richard amedai ana uwezo wa kuziba pengo la Bernard Morrison pale Yanga.

Morrison kwa sasa amekuwa katika mtifuano na klabu yake ya Yanga na inadai bado nyota huyo ni mchezaji halali wa timu hiyo lakini yeye ameshatambulishwa Simba na jana jioni kesi yake ilikuwa inaamuliwa Shirikisho la Soka la Tanzania.

Richard msimu uliopita wa Ligi Kuu alifunga mabao manane huku akiwa mmoja wa wachezaji waliofunga Hat trik kwenye mashindano hayo.

Anasifika kwa kasi na uwezo wake wa kufunga mabao na kushambulia pia kupiga mipira ya faulo ambayo mara nyingi amekuwa mpigaji kwenye kikosi cha Alliance.

Akizungumza na Mwanaspoti, Richard alisema yeye anaamini kiwango chake, hivyo yuko tayari kukipiga Yanga au timu yoyote itakayotaka kumsajili kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu.

Alisema kwa sasa yuko jijini Mwanza na tayari ameshapata ofa nyingi lakini kwake anaangalia timu itakayoweza kumlipa masilahi zaidi ndio maana hajasaini mkataba wowote mpaka sasa.

“Mimi Yanga, Simba au klabu yoyote naweza kucheza pasipo kuhofia namba tena nina imani nikicheza hizi timu nitakuwa bora zaidi kwani ndoto yangu ni kuja kuchezea hizi klabu,” alisema Richard.

Hata hivyo, Winga huyo alisema kwake msimu uliopita ulikuwa wa mafanikio makubwa kwani aliweza kucheza mechi 30 za Ligi Kuu na alikuwa akicheza kwa mara ya kwanza.