Diamond atua studio za Swizz Beatz Marekani

Muktasari:

Msanii wa muziki wa Bongo Fleva nchini Tanzania,Diamond Platnumz, ameonekana akiwa katika studio za mtayarishaji maarufu wa muziki nchini Marekani, Swizz Beatz

Msanii wa muziki wa Bongo Fleva nchini Tanzania,Diamond Platnumz, ameonekana akiwa katika studio za mtayarishaji maarufu wa muziki nchini Marekani, Swizz Beatz.
Hilo linatokea ikiwa ni siku chache zimepita tangu mtayarishaji huyo, aweke wimbo wa ‘Gere’ ulioimbwa na Tanasha Donna akimshirikisha Diamond na ile ya singeli ya ‘Wanga’ iliyoimbwa na Meja Kunta akimshirikisha Lavalava wa lebo ya WCB katika ukurasa wake kwenye mtandao wa Instagram.
Kama haitoshi siku sita zilizopita mtayarishaji huyo aliweka video katika ukurasa wake ikimuonyesha  mwanamuziki Alicia Keys ambaye ni mke wake akionekana kucheza wimbo wa Wanga.
Diamond katika picha hiyo ameonekana amekaa kwenye kiti akiwa amevaa fulana ya njano wakati Swizz Beatz yeye aliyejiegesha kwenye moja ya mashine ndani ya studio hiyo akiwa amevaa tracksuit ya rangi ya chungwa na kofia yenye rangi ya kaki.
Katika picha hiyo, Diamond ameandika ’Kanda! Kanda! nipo na mfalme ananifanya nijisikie kama nipo nyumbani Tanzania, najisikia kama  LasAngelos  ni nyumbani kwangu pa pili”.
Pia picha nyingine imemuonyesha Meneja wa msanii huyo, Babu Tale akiwa na msanii Alicia Keys,picha ambayo Tale ameiweka kwenye ukurasa wake.