Beki Evra azitamani pesa anazopiga Samatta Aston Villa aingia chimbo

Muktasari:

Beki Evra amesema mafanikio ya Samatta yamempa nguvu kubwa ya kujituma kwani anaamini kama akipambana basi naye siku moja anaweza kucheza Ulaya katika ligi kubwa.

Mwanza. Beki wa kushoto wa Polisi Tanzania, Yassin Mustapha ‘Evra’ amesema mafanikio ya Mbwana Samatta ndani ya Aston Villa yampe morari naye kutamani kufika anga za Ulaya.

Evra alisema mafanikio ya Samatta yamempa nguvu kubwa ya kujituma kwani anaamini kama akipambana basi naye siku moja anaweza kucheza Ulaya katika ligi kubwa.

Alisema Samatta amewapa morali kubwa wao wachezaji wa kibongo kufanya vizuri na sasa anacheza katika Ligi Kuu England.

Evra alisema Straika huyo kwa sasa anapiga pesa ndefu kwa kuwa alijituma na kuheshimu mchezo wa soka hivyo nao wanatakiwa kufuata nyayo zake za mafanikio.

“Namfuatilia Samatta nimeona kumbe hakuna linaloweza kushindikana kama ukijituma basi unaweza kupiga pesa za maana Ulaya ili limenipa somo kubwa sana kikubwa nitaendelea kujituma ili nipate mafanikio kama ya nahodha wetu wa timu ya Taifa,”alisema Evra.

“Mpira ndio maisha niliyoyachagua kwa sasa hivyo ni lazima nifanye hii kazi kwa malengo kwangu napambana kuhakikisha natimiza mikakati niliyojiwekea moja wapo ni kucheza soka la kulipwa Ulaya au Afrika kwenye klabu kubwa,” alisema beki huyo wa zamani wa Stand United na Mwadui FC.