Azam, TP Mazembe mtoto hatumwi dukani

Muktasari:

Mazembe katika soka la Afrika wanasifika kwa soka zuri na ubabe hasa baada ya kufanya vizuri katika Mashindano ya Afrika kwa mara kwa mara.

Dar es Salaam. Leo ndio leo katika Kagame Cup, mabingwa watetezi Azam watakuwa na kibarua kigumu mbele ya TP Mazembe wenye rekodi nzuri katika soka la Afrika.

Mazembe katika soka la Afrika wanasifika kwa soka zuri na ubabe hasa baada ya kufanya vizuri katika mashindano ya Afrika kwa mara kwa mara.

Huku Azam inayonolewa na Ettiene Ndayiragije, kocha huyo atakuwa na kibarua kigumu cha kutetea kombe hilo (bingwa mtetezi) mbele ya TP Mazembe.

Mazembe ina nyota wake kama Rainford Kalaba ambaye anasifika kwa uwezo mkubwa wa kumiliki mpira pamoja na spidi yake ya kupeleka mashambulizi kwa timu pinzani.

Azam yupo Idd Nado ambaye naye ni mwepesi katika kupeleka mashambulizi kwa timu pinzani, lakini anabidi aonyeshe ukomavu mbele ya mabeki wa Mazembe ambao wamezoea kukutana na washambuliaji wa kila aina katika kombe la klabu bingwa barani Afrika.

Mchezo wa huo unatarajia kupigwa saa kumi na moja jioni kwa saa za Afrika Mashariki, huku robo fainali ya pili KCCA FC dhidi ya Rayon Sports ikipigwa saa moja na nusu.

NYOTA AFUNGUKA

Kiungo wa Azam Fc, Masoud Abdallah ‘Cabaye’ alisema katika mchezo huo utakuwa mgumu kwa pande zote kutokana na kila timu inataka kuvuka kwenda katika hatua inayofuata.

“Mechi ni ngumu tunacheza na timu kubwa na ina wachezaji wazoefu wengi, lakini uzuri utakuwepo  kwasababu na sisi tumejiandaa vizuri tutaenda kufanya kile mwalimu ametaka tufanye,” alisema Cabaye.