Kocha Amri Said alia ubinafsi unaiangamiza Biashara United

Muktasari:

Biashara United imepoteza michezo yote miwili mfululizo tangu kaunza kwa Ligi Kuu Bara msimu huu dhidi ya Kagera Sugar na Mbao.

Dar es Salaam.Baada ya kupoteza mechi mbili mfululizo kocha wa Biashara United, Amri Said amesema hawatakubali kupoteza tena mchezo ujao dhidi ya Alliance FC utakaofanyika Ijumaa kwenye Uwanja wa Nyamagana Mwanza.

 Amri alisema papara na ubinafsi wa wachezaji wake umechangia kupata matokeo hayo katika michezo hiyo huku wao wakishindwa kufunga bao hata moja.

Kocha huyo wa zamani wa Lipuli amesema katika michezo hiyo moja ya mapungufu aliyoyaona ni kukosa umakini katika umaliziaji na ubinafsi wa baadhi ya wachezaji wake pindi wanapokuwa katika nafasi nzuri ya kufunga.

Amri alisema wanaendelea kujifua kwa ajili ya mchezo wao dhidi ya Alliance utakaofanyika Ijumaa wakiwa na malengo ya kuhakikisha wanashinda.

"Michezo iliyopita yote miwili tumepoteza hivyo hatutaki kupoteza tena tunataka kuhakikisha tunashinda huko huko ugenini na naamini wachzaji wangu watabadilika na kuweza kuipa timu ushindi," alisema Amri.

"Ukiangalia kitu kinachotunyima mabao ni umakini mbovu wa umaliziaji kwa wachezaji wangu na baadhi pia ni wabinasi pale wanapolifikia lango la wapinzani.

"Baadhi ya wachezaji wangu mara nyingi wanapofika kwenye eneo la hatari kila mmoja anaamini yeye anaweza kumalizia na kufunga kabla ya kumpa mwenzake pasi ambaye kwa wakati huo anakuwa katika nafasi nzuri zaidi. Jambo hilo nalendelea kulifanyio kazi kabla ya kukutana na Alliance ili kuhakikisha tunapata mabao mengi katika mchezo huo.