Harmonize, Babu Seya, Mboni wafunga ndoa ndani saa 48

Muktasari:

Mastaa hao ni mwanamuziki mkongwe Nguza Viking maarufu Babu Seya , Rajab Abdul 'Harmonize' wa bongo fleva na mtangazaji wa kipindi cha The Mboni Show, Mboni Masimba.

Dar es Salaam. Mastaa watatu wameandika historia ya kufunga ndoa ndani ya saa 48, wawili kati yao wakifanya sherehe ukumbi mmoja.

Mastaa hao ni mwanamuziki mkongwe Nguza Viking maarufu Babu Seya , Rajab Abdul 'Harmonize' wa bongo fleva na mtangazaji wa kipindi cha The Mboni Show, Mboni Masimba.

Aliyefungua dimba ni Mboni  aliyefunga ndoa na mwanamume anayedaiwa kuishi Marekani anajulikana kwa jina la Ally, ambaye alivalishwa pete siku ya Alhamisi ya Septemba 5, 2019  na kufunga ndoa Ijumaa ambayo sherehe ilifanyika Ukumbi wa  Serena Hotel, akifuatiwa na Hamorinize aliyefunga ndoa na mpenzi wake wa siku nyingi Sarah, katika ukumbi huo huo.

Babu Seya alifunga ndoa na Esterine Haule ambaye ni Katibu Tawala wa Wilaya Muheza (DAS) katika Kanisa Katoliki lililopo Sinza Palestina jijini Dar es Salaam.

Babu Seya aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akisema mchumba wake huyo walikutana baada ya kutoka jela mwaka 2017 huku akiwa na baraka zote kutoka kwa watoto wake kufunga ndoa.

Kuhusu ndoa ya Harmonize, katika mitandao ya kijamii zimesambaa habari za madai kuwa wasanii wa Lebo ya Wasafi inayoongozwa na mwanamuziki Diamond Platinumz, hawakuhudhuria na kudai huenda sababu ni ule mpango wa Harmonize kutaka kujitoa katika lebo hiyo.

Hata hivyo kwa upande wa Diamond kwa sasa yuko nchini Ujerumani ana shoo ambapo ameongozana na Meneja wake Sallam SK.