Wanyama atoswa kweupee hapo Tottenham Spurs

Muktasari:

Kiungo huyo wa kimataifa wa Kenya anahusishwa na mpango wa kuhamia Club Bruges ya Ubelgiji kwa ada ya Pauni 10 milioni.

London, England. Mauricio Pochettino ni kama anamsukumia nje na mabegi yake kiungo Victor Wanyama kwa kumwambia kwamba maisha yake huko Tottenham Hotspur yameshafika mwisho na kusisitiza kwamba wao hawatoi hisani.
Kiungo huyo wa kimataifa wa Kenya anahusishwa na mpango wa kuhamia Club Bruges ya Ubelgiji kwa ada ya Pauni 10 milioni. Pochettino, ambaye ataiongoza Spurs kwenye mechi yake ya 500 tangu alipokuwa kocha wa kikosi hicho watakapomenyana na Newcastle United kwenye Ligi Kuu England leo Jumapili, alisema kitu pia kuhusu kiungo Christian Eriksen kuwa hajui kama atabaki au ataondoka wakati dirisha la usajili wa Ulaya litakapofungwa Septemba 2. Pochettino alisema kuhusu Wanyama kwamba hatasimama njiani kuzuia uhamisho wa mchezaji huyo kama maofisa wa Spurs watafikia makubaliano na Bruges. Kocha huyo aliyewahi kumwelezea Wanyama kuwa “mnyama” huko nyuma kutokana na soka lake la kibabe ndani ya uwanja, alisema kwa sasa haoni kama mchezaji huyo atapata nafasi tena kikosini, akisema: “Yote hii ni kuhusu ubora wa uwanjani. Soka la leo na kesho, haliweza kuwa kama la jana. Unahitaji kuonyesha kwamba kweli unastahili kubaki. Ishu ya Victor, amekuwa akipata sana majeruhi, wenzake wakaibuka kuchukua nafasi. Hii ni timu, hatutoi hisani.
“Nataka kuweka sawa hapa, maneno haya si kuhusu Victor, lakini sisi hatutoi hisani. Kiwango ndio mpango mzima na wachezaji ni wengi.”
Pochettino, ambaye anatarajia kumrejesha kikosini kiungo Dele Alli alisema siku zote amekuwa akiwaambia wachezaji wake wasisumbuliwe na kitu kinachoitwa uvumi.