Kwa mkeka huu wa Savage, Arsenal anakufa Anfield!

LONDON, ENGLAND
KOCHA, Unai Emery amesema kwamba dawa ya moto ni moto, hivyo watawashushia Liverpool mziki mnene kwenye mchezo wao wa Ligi Kuu England utakaopigwa huko Anfield kesho Jumamosi.
Kwenye mchezo huo, kocha Emery amepanga kupanga washambuliaji wake wote matata, Pierre-Emerick Aubameyang, Alexandre Lacazette na Nicolas Pepe huku akitarajia kumrudisha kwenye kikosi kiungo wa Kijerumani, Mesut Ozil.
Arsenal wanafahamu wazi mara ya mwisho walipokwenda Anfield walikumbana na kipigo kizito, Bao Tano, hiko kocha Emery anaamini kumleta David Luiz kwenye beki kutamaliza tatizo, licha ya gwiji mmoja wa wababe hao wa Emirates, Charlie Nicholas kuamini kwamba mechi hiyo itakuwa ubatizo wa moto kwa beki huyo Mbrazili kutokana na makali ya fowadi ya Liverpool inayoundwa na Mohamed Salah, Sadio Mane na Roberto Firmino.
Arsenal na Liverpool zote zimeshinda mechi zao za kwanza, wakivuna pointi sita katika mechi mbili, lakini sasa watakutana wenyewe kwa wenyewe katika wikiendi ya tatu ya Ligi Kuu England, ikishuhudia mechi za vigogo wa Big Six, baada ile ya Manchester United na Chelsea kwenye wikiendi ya kwanza, kisha ya Manchester City na Tottenham kwenye wikiendi ya pili. Wikiendi hii, Man City wao watacheza na Bournemouth na Man United watakipiga na Crystal Palace. Chelsea ya Frank Lampard itakwenda kuikabili Norwich City ya kiboko ya mabao Teemu Pukki huko Carrow Road.
Newcastle United watakuwa na shughuli pevu kuwakabili Spurs, ambapo Heung-Min Son huenda akacheza mechi hiyo, wakati Aston Villa ya Dean Smith yenyewe ilimalizana na Everton usiku wa leo Ijumaa. Wolves watakipiga na Burnley.
Sheffield United watakuwa nyumbani wikiendi hii kuwakabili Leicester City, huku Southampton wakiwafuata Brighton.
Wakati hilo likiendelea, staa wa zamani kwenye Ligi Kuu England, Robbie Savage yeye ametoa utabiri wake kuhusu mechi hizo na huu hapa ndio mkeka wake.
Aston Villa 1-2 Everton
Norwich 1-2 Chelsea
Brighton 2-1 Southampton
Man United 3-0 Crystal Palace
Sheff Utd 2-2 Leicester
Watford 1-1 West Ham
Liverpool 3-1 Arsenal
Bournemouth 0-3 Man City
Tottenham 2-0 Newcastle
Wolves 2-1 Burnley