Mwasapili, Mapunda wampa jeuri kocha Mwambusi wa Mbeya City

Muktasari:

Mwasapili na Mapunda nimefanya nao kazi kwa mafanikio nina imani kurudi kwao wamefanya uamuzi sahihi watakuwa chachu ya mafanikio yangu tena kwa msimu mpya unaotarajia kuanza hivi karibuni na sisi kuanza na wapinzani wetu

USAJILI wa kipa Aaron Kalambo, beki Hassan Mwasapili na mshambuliaji Peter Mapunda ndani ya Mbeya City umemtia kiburi Kocha Juma Mwambusi akiamini wataongeza chachu ya mafanikio msimu huu wa 2019-2020.
Kocha Mwambusi aliliambia Mwanaspoti kuwa, kurudi kwa nyota hao ambao baadhi yao aliwahi kufanya nao kazi kutawaongezea ubora na nguvu vijana wake, huku akifichua Kalambo ni chaguo sahihi langoni kutokana na kipaji alichonacho.
Mwambusi alisema yeye ni muumini wa vijana na kikosi chake kimetawaliwa na chipukizi waliopandishwa kutoka timu ya vijana na wengine wamesajiliwa chini ya mapendekezo yake, hivyo haoni cha kumzuia kuwasha moto mkali msimu huu unaoanza Agosti 24.
“Mwasapili na Mapunda nimefanya nao kazi kwa mafanikio nina imani kurudi kwao wamefanya uamuzi sahihi watakuwa chachu ya mafanikio yangu tena kwa msimu mpya unaotarajia kuanza hivi karibuni na sisi kuanza na wapinzani wetu,” alisema na kuongeza kuwa:
“Ujio wa aliyekuwa kipa namba moja wa wapinzani wetu Tanzania Prisons unazidisha changamoto ya makipa langoni ukizingania ni mchezaji ambaye tayari ameshawahi kujumuishwa katika kikosi cha timu ya taifa.”
Mwambusi alisema anajivunia usajili mkubwa alioufanya anaamini atafanya vitu vikubwa msimu ujao katika Ligi Kuu huku akibainisha kuwa hafanyi kwa kuamini katika historia, bali anapambana kuona anarudisha heshima katika klabu hiyo na kuwarudisha Wanambeya kuishangilia timu yao.