Kocha Villa asema Samatta bado kidogo tu

Muktasari:

Samatta amecheza kwa mafanikio makubwa klabu za Simba, TP Mazembe na Genk ambako alikuwa mpachika mabao tegemeo.

Birmingham, England.NAHODHA wa Taifa Stars, Mbwana Samatta amebakiza hatua chache tu kukamilisha dili lake la kujiunga Aston Villa.
Kwa sasa ndio usajili unaosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka kwenye kila kona ya Tanzania.
Tayari Samatta yuko jijini Birmingham, Uingereza ambako ndio makao makuu wa Aston Villa yalipo, akifanyiwa vipimo wakati taratibu zingine za kimkataba zikiendelea.
Kocha wa Aston Villa, Dean Smith ambaye anataka kumuona Samatta akijiunga haraka ili kusaidia kuiokoa timu hiyo isishuke daraja, amesema: "Tuko karibu kabisa kukamilisha usajili wa Samatta. Kama tukimaliza kila kitu basi ataanza kazi mara moja kwa sababu ni mchezaji mzuri na ana nidhamu nzuri pia”
Dean alikuwa akizungumza muda mfupi baada ya mchezo kati ya Aston Villa na Brighton ambao ulimalizika kwa sare ya bao 1-1 jana Jumamosi.
Aston Villa imnatarajiwa kumtambulisha Samatta kuwa mchezaji wake mpya muda wowote baada ya taratibu kukamili.
Akiwa Genk ambao tayari wamshamuaga na kumpa Baraka zote, Samatta aliifungia mabao 43 katika mechi 98 za Ligi Kuu Ubelgiji. Pia, amefunga mabao mengine kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Dean analazimika kugeukia huduma ya Samatta, ambaye alikuwa mshambuliaji tegemeo la Genk baada ya kuumia kwa mpachika mabao wake, Wesley anayetarajiwa kuwa nje hadi mwishoni mwa msimu.