Staa Man United aamriwa kutumikia kifungo jela
Muktasari:
- Mahakama nchini Brazil imetoa uamuzi huo, huku ikisema kwamba ikiwa hatatoa kiasi hicho, atafungwa.
BRASILIA, BRAZIL: Mchezaji wa zamani wa Manchester United, Anderson Luís de Abreu Oliveira maarufu kama Anderson ameamriwa kutumikia kifungo cha siku 30 jela iwapo hatatoa kiasi cha Pauni 142,000 kwa ajili ya malezi ya watoto wake.
Mahakama nchini Brazil imetoa uamuzi huo, huku ikisema kwamba ikiwa hatatoa kiasi hicho, atafungwa.
Taarifa zinaonyesha kwamba Anderson alijulishwa kuhusu uamuzi huu mwanzoni mwa Septemba, lakini habari imetolewa hivi karibuni. Anderson atakabiliana na kifungo gerezani, lakini akilipa kwa kuchelewa ataruhusiwa kutoka gerezani mchana kwa ajili ya kufanya kazi za kijamii kabla ya kurudi usiku.
Anderson pia anachunguzwa kwa tuhuma za kuhusika katika utakatishaji wa fedha kiasi cha Pauni 4.7 milioni kupitia sarafu za kidijitali. Gazeti la Brazil, Globo, limeeleza kwamba Anderson ni miongoni mwa watu wanane walioo chini ya uchunguzi.
SAFARI YAKE KISOKA
Anderson alianza soka katika timu ya Gremio nchini Brazil kabla ya kusainiwa na Porto akiwa na umri wa miaka 17 kwa kiasi cha Euro 7 milioni. Ili kufanikisha uhamisho huo, wazazi wake walihamia Ureno.
Katika msimu wa 2006/07 alicheza mara ya kwanza Ligi ya Mabingwa Ulaya, lakini akakumbana na majeraha. Manchester United walimfuatilia na kumnasa mwaka 2007 kwa Pauni 20 milioni.
Kutokana na umahiri wake alipewa jezi namba 8, na baada ya mwaka mmoja alinyakua ubingwa wa Ulaya akiwa na Mashetani Wekundu akifunga penalti muhimu katika ushindi wa 6-5 dhidi ya Chelsea.
Mwaka wa 2008 ulikuwa wa mafanikio kwake aliposhinda tuzo ya Golden Boy na kufunga penalti ya ushindi katika fainali ya Kombe la Ligi. Lakini mwaka uliofuata alikabiliwa na matatizo ya kinidhamu na majeraha, jambo lililomfanya kupoteza nafasi yake Old Trafford.
Baada ya kuondoka Manchester United 2015 alijiunga na Internacional kabla ya kustaafu 2020 akiwa na umri wa miaka 31.