Staa Isak hataki kutoa visingizio
Muktasari:
- Isak, ambaye amesajiliwa na Liverpool kwa ada ya Pauni 130 milioni, amefunga bao moja tu kwenye klabu yake hiyo mpya tangu alipojiunga na miamba hiyo ya Anfield kwenye siku ya mwisho ya kufungwa kwa dirisha la usajili wa majira ya kiangazi.
LIVERPOOL, ENGLAND: STRAIKA Alexander Isak amesema hana cha kujitetea juu ya kiwango kibaya kwenye mwanzo wa maisha yake huko Liverpool.
Isak, ambaye amesajiliwa na Liverpool kwa ada ya Pauni 130 milioni, amefunga bao moja tu kwenye klabu yake hiyo mpya tangu alipojiunga na miamba hiyo ya Anfield kwenye siku ya mwisho ya kufungwa kwa dirisha la usajili wa majira ya kiangazi.
Isak alirejea uwanjani akitokea kwenye maumivu ya misuli ya kinena akitokea benchi kwenye mechi ya Sweden iliyochapwa mabao 4-1 na Uswisi, alishindwa hata kupiga shuti.
Isak amekosekana uwanjani tangu Oktoba 22 kutokana na kuwa majeruhi na bado hajaanzishwa kwenye mechi yoyote. Baada ya kutumikia sehemu kubwa ya pre-season akifanya mazoezi kivyake wakati alipokuwa akilazimisha uhamisho wake wa kwenda Anfield, hadi sasa bado hajaonyesha kiwango bora kabisa ndani ya uwanja.
Bao pekee la Isak alilofunga hadi sasa alifanya hivyo dhidi ya timu inayotaabika kwenye Championship, Southampton kwenye Kombe la Ligi, lakini amekuwa na matumaini makubwa ya kurudi kwenye kiwango chake bora ndani ya uwanja.
Isak amesema: “Mambo si mazuri. Lakini, ninapokuwa uwanjani, huwa sitoi kisingizio chochote. Siku zote nataka kucheza mchezo wangu na kuonyesha kiwango. Ni ngumu sana kuwa mbali na kushindwa kusaidia timu. Sasa nimerudi na nipo sawa tu.
“Hakuna urahisi kwenye soka. Lakini, huu ni uzoefu ambao unapata ili kupambana na vitu. Inahuzunisha sana unapokuwa majeruhi. Haijalishi ni mechi moja au zaidi. Siku zote inakuwa mbaya sana kwa mchezaji mwenyewe.”
Mchezaji mwenzake Isak huko kwenye timu ya taifa ya Sweden, Anthony Elanga, ambaye alijiunga na Newcastle United kabla ya Isak hajaondoka St James’ Park, amesema anaamini straika huyo wa Anfield atakuwa fiti na kurejea kwenye makali yake. Elanga amesema:
“Tunafahamu ubora wa Alex na sota tunamwaamini na tuna imani naye. Ni mchezaji wa kiwango cha juu. Huwezi kugharimu pesa nyingi vile na unakwenda kujiunga na timu kama Liverpool halafu usiwe na mchezaji mzuri. Ni suala tu la kuwa na imani naye na kumpatia muda kwa sababu atakuwa vizuri.”