Paul Pogba abeba tuzo, amshukuru Ronaldo
Muktasari:
- Mchezaji huyo amekuwa akipata nafasi ya kucheza katika klabu yake mpya ya Monaco wakati huu akiwa anapambana kwa nguvu zote kurudi kwenye ubora wake baada ya kuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu kutokana na kufungiwa kulikotokea na kufeli kwenye vipimo vya dawa za kusisimua misuli.
MONACO, UFARANSA: KIUNGO wa Monaco, Paul Pogba amemshukuru sana Cristiano Ronaldo baada ya kupokea tuzo yake ya Best Comeback Award katika sherehe za Globe Soccer Awards 2025 zilizofanyika Dubai, Falme za Kiarabu.
Mchezaji huyo amekuwa akipata nafasi ya kucheza katika klabu yake mpya ya Monaco wakati huu akiwa anapambana kwa nguvu zote kurudi kwenye ubora wake baada ya kuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu kutokana na kufungiwa kulikotokea na kufeli kwenye vipimo vya dawa za kusisimua misuli.
Pogba, 32, aliruhusiwa kuanza mazoezi Januari 2025, lakini alisubiri hadi kwenye majira ya kiagazi kusainiwa na timu hiyo ambayo inajaribu kumrudisha mkali huyo wa zamani wa Manchester United na Juventus kwenye makali yake.
Pogba ameshinda tuzo ya Best Comeback Award kwenye Globe Soccer Awards 2025 zilizofanyika Dubai mwaka huu, ambapo alitambulika kwa uchapaji wake kazi katika mchakato wa kurudi kwenye mikikimikiki ya soka la kulipwa.
“Haikuwa rahisi. Kilikuwa kipindi muhimu kwangu, katika maisha yangu kuona watu wanachukuliane, nani anayekupenda kwa dhati. Tuzo hii ina maana kubwa sana, kwangu na kwa mke wangu. Tumevuka kwenye mapito haya pamoja. Alinisaidia sana na watoto wangu walinifanya nitabasamu.”
Kisha Pogba alimshukuru Ronaldo, akiamini kwamba amemhamasisha kila mwanasoka baada ya kutamba kwenye soka la kiwango cha juu kwa zaidi ya miongo miwili.
Pogba aliongeza akisema kuwa, “Cristiano upo hapa, umetuhamasisha sisi wote kama mchezaji wa soka. Umefanya hili kwa ajili ya kizazi kijacho. Asante sana Cristiano.”