Paul Pogba kurudi dimbani baada ya mwaka mmoja
Muktasari:
- ESPN imeripoti kuwa, bechi la ufundi la AS Monaco lina mpango wa kumchezesha Pogba kwa dakika chache tu, kwenye mechi hiyo ya Ligi Kuu ya Ufaransa.
Kiungo wa Ufaransa, Paul Pogba anatarajiwa kucheza mechi yake ya kwanza akiwa na AS Monaco kesho Jumamosi, Novemba 22, 2025 dhidi ya Rennes, huku akiendelea kujiandaa kurejea katika mechi za ushindani.
ESPN imeripoti kuwa, bechi la ufundi la AS Monaco lina mpango wa kumchezesha Pogba kwa dakika chache tu, kwenye mechi hiyo ya Ligi Kuu ya Ufaransa.
Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 32, mara ya mwisho alicheza dakika 28, Septemba 3, 2023, akiwa na Juventus dhidi ya Empoli.
Agosti 2023, Pogba alikutwa na hatia ya kutumia dawa za kusisimua msuli aina ya DHEA, hali ambayo ilipelekea kufungiwa kucheza soka kwa miaka minne mnamo Februari 2024.
Hata hivyo, adhabu hiyo ilipunguzwa hadi miezi 18, baada ya Pogba kukata rufaa katika Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS).
Pogba alifanya mazoezi kama kawaida na kikosi cha AS Monaco jana Alhamisi, Novemba 20, 2025 na leo Ijumaa Novemba 21, 2025 atafanya mazoezi ya mwisho na wachezaji wenzake.
Kama hakutakuwa na matatizo yoyote baada ya mazoezi hayo, Mfaransa huyo atasafiri kwenda Rennes tayari kwa mecdhi ya kesho Jumamosi, Novemba 22, 2025.
Kiungo huyo wa zamani wa Manchester United, alitarajiwa kucheza dhidi ya Angers kabla ya mapumziko ya kimataifa, lakini alipata jeraha dogo la kifundo cha mguu mazoezini na kulazimika kukosekana.