Osimhen kumrithi Harry Kane Bayern Munich
Muktasari:
- Nahodha huyo wa timu ya taifa England kwa sasa ana umri wa miaka 32, na kumekuwa na minong’ono mingi kuhusu hatma yake kwani haonekani kuwa na zaidi ya misimu mitatu mbele ya kuitumikia timu hiyo.
MUNICH, UJERUMANI: BAYERN Munich inaripotiwa kuongeza kasi katika mpango wao wa kumsajili straika wa Galatasaray, Victor Osimhen, ikiwa ni katika kujiandaa na maisha bila ya staa wao Harry Kane ambaye umri umeshaanza kumtupa mkono.
Nahodha huyo wa timu ya taifa England kwa sasa ana umri wa miaka 32, na kumekuwa na minong’ono mingi kuhusu hatma yake kwani haonekani kuwa na zaidi ya misimu mitatu mbele ya kuitumikia timu hiyo.
Vilevile inaelezwa, kocha wa Bayern Vincent Kompany inadaiwa ana hamu kubwa ya kuhakikisha nyota huyo wa kimataifa wa Nigeria anayeng’ara kwa sasa akiwa Galatasaray anakuwa mrithi wa Kane katika viunga vya Allianz Arena.
Kwa mujibu wa FootMercato, Kompany amekuwa akimfuatilia mshambuliaji huyo wa zamani wa Lille tangu akiwa Charleroi.
Licha ya Kane kuendelea kutawala kama mfungaji bora wa Bayern msimu huu akiwa na mabao 45 katika mechi 37 kwenye mashindano yote, dili la Osimhen linachukuliwa kwa uzito mkubwa na mabosi wa timu hiyo.
Hata hivyo, kupata saini ya Osimhen haionekani kuwa rahisi kwa mabingwa hao wa Ujerumani kwani Galatasaray ambayo ilibadili dili lake la mkopo kuwa la kudumu kwa kulipa Euro 75 milion, kudai mchezaji huyo atauzwa kwa bei kubwa zaidi ya ile aliyonunuliwa nayo.
Wakati Bayern wakiongeza juhudi za kutaka kumsajili staa huyo, Paris Saint-Germain ambayo iliripotiwa kutaka kumsajili hapo awali inadaiwa kufunga mlango wa dili hilo.
Mabingwa hao wa Ufaransa wamekatishwa tamaa baada ya kugundua Galatasaray itahitaji zaidi ya Euro 150 milioni ili kumuuza fundi huyo ambaye pia anahitaji mshahara usiopungua Euro 20 milioni kwa mwaka.