Mastaa wa kutazamwa AFCON 2025
Muktasari:
- KWA wingi wa vipaji vya Afrika vitakavyokuwa Morocco kwenya mashindano ya Afcon 2025, kuna orodha ya mastaa ambao wanaaminika watakwenda kuwa kivutio kikubwa katika mikikimikiki hiyo.
RABAT, MOROCCO: KWA wingi wa vipaji vya Afrika vitakavyokuwa Morocco kwenya mashindano ya Afcon 2025, kuna orodha ya mastaa ambao wanaaminika watakwenda kuwa kivutio kikubwa katika mikikimikiki hiyo.
Kundi A
Morocco – Brahim Diaz
Katika soka la Afrika, Morocco imekuwa kinara miaka ya hivi karibuni, ikifika nusu fainali ya Kombe la Dunia 2022 na kushinda CHAN 2024. Timu yao ya wakubwa ina nyota wengi na Brahim Diaz yuko juu katika orodha hiyo. Baada ya kubadili uraia kutoka Uhispania mwaka 2024, nyota huyo wa Real Madrid amekuwa mhimili, akifunga mabao saba kwenye mechi nne za kufuzu Afcon 2025. Akiwa na Achraf Hakimi nyuma yake, anapata nafasi zaidi kutumia ustadi wake wa kumiliki mpira na kupita mabeki. Akicheza nyumbani, tegemea ataonekana sana.
Mali – Dorgeles Nene
Safari ya Dorgeles Nene barani Ulaya imepita Austria, Ubelgiji hadi Uturuki ambako sasa anatamba na Fenerbahce.
Kimo chake, kasi yake na uwezo wa kucheza pande zote za uwanja wa mbele humfanya kuwa tishio. Anaweza kusababisha matatizo kwa mabeki kwenye michuano hii.
Zambia – Patson Daka
Ikiwa nafasi ya 90 duniani, Zambia ina vipaji vichache, lakini nyota wao ni Patson Daka.
Licha ya kutofunga sana kwenye klabu, kwa taifa amekuwa bora zaidi na ana mabao matatu kwenye mechi saba za kufuzu Kombe la Dunia mwaka huu. Akiwa anakamilisha mkataba Leicester City, Afcon 2025 inaweza kuwa jukwaa la kujiuza tena.
Comoros – Rafiki Said
Comoros imefuzu AFCON kwa mara ya pili katika historia yake. Ulinzi umekuwa silaha yao, lakini Rafiki Said ndiye tishio mbele. Amefunga mabao muhimu kwenye mechi za kufuzu na ana mabao manane kwenye mechi 17. Anaonekana kama mustakabali wa timu hii katika mashindano hayo ya Morocco.
Kundi B
Afrika Kusini – Teboho Mokoena
Amefikia mechi 50 za kimataifa na ni mhimili wa timu. Akiwa na uzoefu mkubwa, aliisaidia Afrika Kusini kumaliza nafasi ya tatu AFCON iliyopita. Kama Bafana Bafana inataka kuandika historia, Mokoena atahitajika sana.
Zimbabwe – Jordan Zemura
Zimbabwe inahitaji nyota wao wanaocheza Ulaya, akiwamo beki wa kushoto, Jordan Zemura anayekipiga katika klabu ya Udinese. Akiwa anacheza kama winga wa kushoto kwa taifa, ubunifu na uwezo wa kupiga mipira iliyokufa ni tishio.
Misri – Trezeguet
Wakati Mohamed Salah na Omar Marmoush wakibeba matarajio ya taifa la Misri katika mashindano ya Afcon 2025, Trezeguet anaweza kuwa kivutio na tishio zaidi. Tangu 2025, amefunga mabao tisa kwenye mechi 15, akionyesha kurejea kwenye ubora wake.
Angola – Fredy
Akiwa na miaka 35, Fredy anaiongoza Angola kwenye AFCON nyingine, akitafuta kuvuka robo fainali kwa mara ya kwanza.
Ameongeza mabao kwenye mchezo wake msimu huu na anaweza kuwa muhimu.
Kundi C
Tanzania – Novatus Miroshi
Tanzania siyo kati ya timu zinazopewa nafasi, lakini Novatus Miroshi anaweza kuwa muhimu. Amechezeshwa sana na Goztepe kwenye Super Lig na ni mkabaji mzuri ambaye hupenda kuanzisha mashambulizi ya kushtukiza.
Nigeria – Christantus Uche
Nigeria inaingia AFCON 2025 ikiwa na shinikizo baada ya kukosa Kombe la Dunia 2026. Christantus Uche, ambaye safari yake kutoka ligi za chini Hispania hadi Ligi Kuu England imekuwa ya kasi, anaweza kuleta kitu kipya kikosini Super Eagles.
Tunisia – Hannibal Mejbri
Akiwa na uzoefu wa kucheza kwenye Ligi Kuu England, Hannibal ni muhimu kwa taifa la Tunisia. Anacheza Namba 10 na licha ya kutokuwa na michango mingi ya mabao, ubunifu wake ni mkubwa na ni muhimu kwa timu yake.
Uganda – Jordan Obita
Akiingia AFCON kwa mara ya kwanza, Obita anaongeza uzoefu mkubwa kwenye ulinzi wa Uganda.
Hata hivyo, kuna wasiwasi kuhusu jeraha la kifundo cha mguu alilopata katika mechi dhidi ya Celtic.
Kundi D
Senegal – Nicolas Jackson
Kwenye timu iliyojaa vipaji, straika Nicolas Jackson anaweza kuwa muhimu. Amefanya vyema Bayern Munich licha ya kukaa benchi mara kadhaa. Atakuwa chaguo muhimu kwenye kikosi cha Senegal katika mashindano hayo ya Afcon 2025.
Botswana – Tumisang Orebonye
Licha ya Botswana kutotarajiwa kufanya makubwa, Orebonye anaweza kuonekana kwa kiwango chake kizuri cha kazi uwanjani na uzoefu nje ya Kusini mwa Jangwa la Sahara.
DR Congo – Chancel Mbemba
Mbemba ana uzoefu mkubwa mechi 101 katika kikosi cha timu ya taifa. Aliongoza safu ya ulinzi na kucheza mechi nne kati ya sita bila ya kuruhusu bao katika mechi za kufuzu huku akiwa moto kwa mipira ya kutengwa.
Benin – Junior Olaitan
Akiwa na miaka 23, Olaitan ni kiungo mbunifu mwenye uwezo wa kutoa pasi muhimu. Atacheza kama Namba 10.
Kundi E
Algeria – Mohamed Amoura
Amoura amekuwa moto, mabao 10 kwenye mechi 10 za kufuzu Kombe la Dunia.
Pia anaonekana kuwa hatari kwenye klabu yake Wolfsburg.
Equatorial Guinea – Saul Coco
Ni beki thabiti ambaye ameonyesha kiwango kizuri Serie A.
Alikuwa sehemu ya kikosi kilichofanya vizuri AFCON iliyopita.
Burkina Faso – Edmond Tapsoba
Nyota mkubwa wa timu, Tapsoba ni beki mwenye utulivu na uwezo wa kupiga pasi ndefu.
Anaweza kucheza hadi kiungo kusaidia timu.
Sudan – Mohamed Abdelrahman
Mfungaji bora wa historia ya Sudan, mabao 13.
Anaweza kuwa kwenye AFCON yake ya mwisho, hivyo atahitajika sana.
Kundi F
Cameroon – Carlos Baleba
Akiwa na miaka 21, Baleba ni mmoja wa wachezaji ghali zaidi.
Ni kama dereva mzuri katika kiungo, mwenye nguvu na mashuti makali.
Gabon – Pierre-Emerick Aubameyang
Huenda hii ikawa nafasi ya mwisho kwa Aubameyang mwenye miaka 36.
Bado ndiye tegemeo la timu timu yake katika fainali hizo za Afcon 2025.
Msumbiji – Reinildo Mandava
Ameonekana akiwa kwenye kiwango bora akiwa na Sunderland na kwa taifa anacheza kama beki wa kati.
Anabeba matumaini ya Msumbiji katika mashindano hayo ya Afcon 2025.
Ivory Coast – Yan Diomande
Licha ya kucheza mechi nne tu za kimataifa, Diomande amekuwa kwenye kiwango bora sana RB Leipzig, akifunga kwenye mechi tatu mfululizo za mwanzo. Ana nguvu, kasi na uwezo wa kucheza pande zote za uwanja.