MAN UNITED YATUPWA NJE CARABAO

Muktasari:
MASHETANI wekundu wa Old Trafford, Manchester United wametupwa nje ya Kombe la Ligi ya England ambalo ni maarufu kama Carabao baada ya kukubali kipigo usiku wa jana, Jumatano cha bao 1-0 dhidi ya wagonga nyundo wa London, West Ham United.
LONDON, ENGLAND. MASHETANI wekundu wa Old Trafford, Manchester United wametupwa nje ya Kombe la Ligi ya England ambalo ni maarufu kama Carabao baada ya kukubali kipigo usiku wa jana, Jumatano cha bao 1-0 dhidi ya wagonga nyundo wa London, West Ham United.
Mshambuliaji wa kimataifa wa Argentina, Manuel Lanzini ndiye aliyeifanya West Ham kuibuka na ushindi wake wa kwanza kwenye uwanja wa Old Trafford tangu 2007 na kuwafanya Manchester United kufangasha virago vyao kwenye michuano hiyo ambayo misimu miwili iliyopita walitinga hatua ya nusu fainali.
Katika mchezo huo, kocha wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer alitoa nafasi kwenye kikosi chake cha kwanza kwa Jadon Sancho na Anthony Martial kuongoza mashambulizi ya timu hiyo lakini walionekana kuchemka ikabidi kuwaingiza Mason Greenwood na Bruno Fernandes.
Licha ya mabadiliko hayo, West Ham ambayo iliwapumzisha baadhi ya nyota wao muhimu kama vile Tomas Soucek, Declan Rice na Michail Antonio walionekana kuwa imara na kumudu presha ya mashambulizi ya Manchester United ambao walikuwa wakisaka bao la kusawazisha.
Wakati Manchester United ikitupwa nje ya michuano hiyo wenzao, Manchester City wametinga raundi ya nne baada ya kuishushia kipigo Wycombe Wanderers cha mabao 6-1, Arsenal nao waliitandika AFC Wimbledon mabao 3-0, Chelsea wamevuka raundi ya tatu baada ya kuifunga Aston Villa kwa penalti 4-3 baada ya kutoka sare ya bao 1-1.
Upande mwingine Liverpool wakiwa ugenini waliitandika Norwich mabao 3-0, kama ilivyokuwa kwa Chelsea, Tottenham nao wametinga raundi ya nne kwa penalti 3-2 baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya wenyeji wao, Wolverhampton Wanderers.
RATIBA YA RAUNDI YA NNE
Chelsea v Southampton
Arsenal v Leeds United
QPR v Sunderland
Stoke City v Brentford
West Ham v Manchester City
Leicester City v Brighton
Burnley v Tottenham Hotspur
Preston North End v Liverpool