Man United, Granada vitani Ulaya
Muktasari:
- BAADA ya robo fainali za michuano ya Ligi ya Mabingwa kupigwa jana na juzi, leo kutakuwa na kimbembe cha robo fainali za Europa League ambapo jumla ya michezo minne inatarajiwa kuchukuwa nafasi katika viwanja vinne tofauti.
GRANADA, HISPANIA. BAADA ya robo fainali za michuano ya Ligi ya Mabingwa kupigwa jana na juzi, leo kutakuwa na kimbembe cha robo fainali za Europa League ambapo jumla ya michezo minne inatarajiwa kuchukuwa nafasi katika viwanja vinne tofauti.
Mechi ambazo zinatarajiwa kutazamwa sana ni kuanzia ile ya Man United na Granada itakayopigwa katika dimba la Estadio Nuevo Los Carmenes nchini Hispania.
Man United itahitaji kushinda mchezo huo ili kujiwekea mazingira mazuri ya kumaliza msimu ikiwa na walau taji moja baada ya hivi karibuni kutolewa kwenye michuano ya FA na Leicester City kwakutandikwa mabao 3-1.
Baada ya mchezo huo wa mkondo wa kwanza ule wa marudiano unatarajiwa kupigwa April 15 mwaka huu.
Mechi nyingine ya kukata na shoka itakuwa kati ya Ajax itakayokuwa nyumbani dhidi ya Roma, wakati Arsenal itakayokuwa London itavaana na Slavia Prague.
Wababe wa Croatia, Dinamo Zagreb watakuwa kwenye viwanja vya kujidai Stadion Maksimir kuialika Villarreal, mechi zote zinatarajiwa kupigwa saa 4:00 usiku.