Havertz aipeleka Arsenal fainali baada ya miaka sita
Muktasari:
- Matokeo hayo yameiwezesha kutinga fainali ya Kombe la Carabao kwa jumla ya mabao 4-2 kufuatia ushindi wa kwanza ugenini wa 3-2.
ARSENAL imefuzu fainali yake ya kwanza baada ya miaka sita kupita kufuatia ushindi wa 1-0 dhidi ya Chelsea katika Uwanja wa Emirates usiku wa Jumanne, Februari 3, 2026, mfungaji akiwa Kai Havertz dakika ya 90+7.
Matokeo hayo yameiwezesha kutinga fainali ya Kombe la Carabao kwa jumla ya mabao 4-2 kufuatia ushindi wa kwanza ugenini wa 3-2.
Mshambuliaji wa zamani wa Chelsea, Kai Havertz, aliihakikishia Arsenal tiketi ya kwenda Uwanja wa Wembley mwezi ujao baada ya kumpita kipa Robert Sánchez na kufunga bao katika dakika za nyongeza za kipindi cha pili.
Baada ya kupoteza mchezo wa kwanza wa nusu fainali nyumbani mwezi uliopita, Chelsea waliwazuia vizuri wapinzani wao wa London kwa sehemu kubwa ya mechi ya marudiano ya Jumanne.
Hata hivyo, kikosi cha Liam Rosenior kilishindwa kutengeneza hatari kubwa langoni ili kupata bao walilohitaji kusawazisha jumla ya mabao, katika mchezo uliokuwa na nafasi chache za kufunga, kabla ya Havertz kufunga bao la ushindi mwishoni.
Katika msimu unaoonekana kuwa wa kipekee kwa klabu hiyo, Arsenal sasa watakutana na mshindi wa nusu fainali nyingine kati ya Manchester City na Newcastle United, katika fainali itakayochezwa Machi 22, 2026. Man City wanaingia kwenye mchezo wa marudiano wa Jumatano leo Februari 4, 2026 wakiwa na faida ya mabao 2-0.
Arsenal wanatafuta kutwaa taji lao la tatu la Kombe la Carabao, baada ya yale ya mwaka 1987 na 1993. Klabu hiyo imewahi kufika fainali mara sita bila kushinda, mara ya mwisho ikiwa ni dhidi ya City mwaka 2018.
Arsenal hawajashinda taji kubwa tangu walipotwaa Kombe la FA mwaka 2020, msimu wa kwanza wa kocha Mikel Arteta akiwa na klabu hiyo.
Kikosi cha Arteta kinaongoza Ligi Kuu ya England kwa tofauti ya pointi sita katika harakati za kutwaa ubingwa wa England kwa mara ya kwanza tangu 2004, na pia kimemaliza juu katika msimamo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kushinda mechi zote nane za hatua ya makundi.
Zaidi ya hayo, Arsenal pia wamefuzu hadi raundi ya nne ya Kombe la FA.
Mchezo wa kwanza wa nusu fainali uliochezwa Stamford Bridge ulikuwa na mabao mengi, lakini kwa kuzingatia nafasi ya kucheza fainali mwezi ujao, mchezo huu ulikuwa wa tahadhari zaidi.
Rosenior, ambaye kabla ya Jumanne usiku alikuwa ameongoza timu yake kushinda michezo mitano mfululizo, alipanga wachezaji watano katika safu ya ulinzi ya Chelsea ili kuizuia Arsenal, na mpango huo ulifanikiwa.
Piero Hincapié ndiye aliyepiga shuti pekee la Arsenal kipindi cha kwanza, akimlazimisha Sánchez kufanya kazi baada ya kupiga shuti la mbali dakika ya 18.
Ubora wa Arsenal kwenye mipira ya adhabu umeonekana sana siku za karibuni. Lakini kila walipopata kona, Chelsea walisukuma wachezaji watatu mbele, huku Arsenal wakilazimika kuwafuata. Mbinu hiyo ilifanya Arsenal kukosa makali yao ya kawaida kwenye mipira ya adhabu.
Kipindi cha kwanza kilivyokaribia kuisha, kipa wa zamani wa Chelsea, Kepa Arrizabalaga ambaye sasa anaidakia Arsenal, aliokoa shuti la mbali la Enzo Fernández.
Kipindi cha pili kilipoanza, Arsenal bado walikuwa na faida, lakini kwa Chelsea kubaki ndani ya tofauti ya bao moja, mvutano wa nusu fainali uliendelea.
Cole Palmer na Estêvão waliingia uwanjani huku Chelsea wakisaka bao la kusawazisha kuweka sawa mzani wa mabao, kabla ya Marc Cucurella na kisha Fernández kujaribu mashuti ya mbali bila mafanikio.
Arsenal walianza kuonekana na presha, na Declan Rice aliwahimiza wachezaji wenzake na pengine hata mashabiki kutulia katika mchezo uliokuwa unazidi kuwa wa vurugu.
Zikiwa zimesalia dakika 14, Gabriel alipata nafasi nzuri ya kuiweka Arsenal salama, lakini kichwa chake kutoka kwenye krosi ya Martin Zubimendi kilizuiwa na Cucurella.
Upande mwingine, mpira wa kichwa wa Wesley Fofana kutoka kwenye kona ulipita karibu na lango la Kepa. Fernández naye alipiga shuti lililopita juu na pembeni katika dakika ya 90, huku kukiwa na dakika sita za nyongeza.
Chelsea walishambulia na kujaribu kila njia, lakini hawakuonekana kuwa na uwezekano wa kupata bao la kuwapeleka kwenye muda wa ziada. Mwishowe, ilikuwa Havertz aliyepokea pasi ya Rice na kufunga kwa utulivu, huku msimu mzuri wa Arsenal ukiendelea kung’ara zaidi.