Guardiola aandaliwa warithi wake Etihad
Muktasari:
- Kocha huyo raia wa Hispania ana mkataba hadi mwisho wa msimu ujao, lakini kikosi chake kimekuwa kikisuasua baada ya mwaka ambao Guardiola amejaribu kukifanyia maboresho kikosi chenye wachezaji waliokuwa wanazeeka.
MANCHESTER, ENGLAND: MANCHESTER City inaandaa mipango ya maisha baada ya Pep Guardiola huku uvumi ukiongezeka huu unaweza kuwa msimu wake wa mwisho katika klabu hiyo ya Etihad.
Kocha huyo raia wa Hispania ana mkataba hadi mwisho wa msimu ujao, lakini kikosi chake kimekuwa kikisuasua baada ya mwaka ambao Guardiola amejaribu kukifanyia maboresho kikosi chenye wachezaji waliokuwa wanazeeka.
Kwa sasa, Man City iko nyuma kwa pointi sita dhidi ya vinara Arsenal na uongozi wa klabu unaanza kuangalia ni nani anaweza kumrithi kocha wao wa sasa.
Ukweli kwamba Enzo Maresca alidai alikuwa na mazungumzo na viongozi wa Man City unaonyesha wazi klabu hiyo tayari inafikiria hatua zao zijazo. Maresca aliwahi kufanya kazi Man City kama msaidizi wa Guardiola, lakini mwezi uliopita alifutwa kazi na Chelsea.
Ripoti zinafichua anatarajiwa kuwa miongoni mwa wanaowania nafasi hiyo ya Etihad.
Xabi Alonso pia yupo kwenye orodha ya wagombea wa kuchukua nafasi ya Guardiola. Mhispaniola huyo aliwahi kucheza chini ya Guardiola alipokuwa Bayern Munich. Amejidhihirisha kama mmoja wa makocha wa kizazi kipya baada ya kuiongoza Bayer Leverkusen kutwaa ubingwa wa Bundesliga bila kupoteza mechi.
Mafanikio hayo yalimsaidia kupata kazi ya Real Madrid, ingawa alidumu kwa nusu msimu pekee kutokana na tetesi za matatizo ya ndani ya klabu. Hata hivyo, hilo halijaharibu sifa yake na bado ni kocha anayehitajika sana. Liverpool huenda ikamsaka Alonso endapo wangeamua kubadilisha kocha wao.
Man City pia inaweza kumzingatia mchezaji mwingine wa zamani wa Guardiola, Cesc Fabregas, huku kazi yake katika klabu ya Como ikiwavutia wengi.
Kwa sasa Como ipo nafasi ya sita kwenye msimamo wa Serie A ya Italia na Fabregas anatarajiwa kuondoka tu iwapo atapata nafasi kubwa katika Ligi Kuu England au Ulaya.
Vincent Kompany pia ametwaa ubingwa wa Bundesliga akiwa na Bayern na anaendelea kufanya kampeni ya kuvutia zaidi msimu huu. Ana historia kubwa na Man City, lakini itakuwa jambo la kushangaza iwapo ataondoka Allianz Arena.
Guardiola ameandika upya historia tangu alipowasili Man City mwaka 2016 akitokea Bayern Munich. Ameshinda mataji sita ya Ligi Kuu England na kuwa kocha wa kwanza kabisa kushinda mataji manne mfululizo. Ubingwa wake wa kwanza pia uliifanya Man City kuwa timu ya kwanza kufikisha pointi 100 katika msimu mmoja wa Ligi Kuu England.