Eti arsenal bingwa? Pep kakataa hilo
Muktasari:
- Ni rahisi tu, kama jeshi hilo la Mikel Arteta litacheza vizuri mechi zake saba zilizosalia, lile paredi lililoandaliwa msimu uliopita la kuzungusha kombe la ubingwa wa Ligi Kuu England safari hii itakuwa kweli.
LONDON, ENGLAND: KAMA unabisha, wewe bisha tu, ila kuna asilimia kubwa Arsenal ikawa bingwa msimu huu, baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Everton, juzi Jumamosi usiku. Hata hivyo, Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola amesema haijaisha hadi iishe na kukataa katakata kuipa miamba hiyo ya Emirates ubingwa.
Ni rahisi tu, kama jeshi hilo la Mikel Arteta litacheza vizuri mechi zake saba zilizosalia, lile paredi lililoandaliwa msimu uliopita la kuzungusha kombe la ubingwa wa Ligi Kuu England safari hii itakuwa kweli.
Hadi sasa Arsenal yenye pointi 70 inaongoza msimu kwa tofauti ya pointi tisa dhidi ya Manchester City yenye 61 na mchezo mmoja mkononi ikiwa imeshacheza 30.
Licha ya sare iliyopata Man City ugenini dhidi ya West Ham United kuinyong'onyesha itatakiwa kushinda mechi zake nane zilizosalia huku ikiombea Arsenal ipoteze zake ikiwamo zitakapokutana Aprili 19, ikiwa nyumbani.
Hata hivyo, Guardiola katika kuonyesha bado hajatolewa kwenye reli ya mbio za ubingwa alisema ubingwa bado ni vita na lolote linaweza kutokea licha ya kuwa nyuma kwa pointi tisa;
"Haijamalizika. Nani alisema hivyo? Hatupotezi uelekeo. Tutaendelea," alisema Guardiola. "Pointi tisa ni nyingi dhidi ya Arsenal lakini imejitokeza. Tuna mechi ya nyumbani hivyo lazima tujaribu hadi mwisho. Wakati ambao ikiwa haitawezekana basi tunampongeza bingwa, lakini lazima tujaribu."
Historia inaonyesha timu pekee iliyoshinda taji la Ligi Kuu England baada ya kumaliza mechi ikiwa angalau pointi tisa nyuma ya viongozi, ikiwa imecheza mechi 30 au zaidi, ni Manchester City msimu wa 2013-14.
Hata hivyo, City kwa sasa haiko katika kiwango cha juu na imepata sare katika mechi zao mbili za mwisho za ligi dhidi ya West Ham, iliyo katika hatari ya kushuka daraja na Nottingham Forest. Pia imetoka kuchakazwa vibaya kwenye kipigo cha mabao 3-0 dhidi ya Real Madrid kwenye mechi ya kwanza ya hatua ya 16 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Baada ya ushindi huo ulioshuhudia kinda wa washika mitutu hao wa London, Max Dowman akihusika na mabao yote mawili, akifunga na kusaidia upatikanaji wa bao, Arteta alisema;
“Miezi michache iliyopita imekuwa ya ajabu. Tunaingia kwenye kila mechi kama ni ya mwisho vile. Wakati mwingine tunaonyesha kiwango kizuri, wakati mwingine wa cha kipekee zaidi,” alisema na kuongeza;
“Lakini hamu ya kushinda, msimu mzima, ndiyo kitu bora zaidi kwa timu hii. Ni jambo ambalo linaonyesha roho ya ushindi.”
Katika mechi dhidi ya Everton, mshambuliaji kinda wa Arsenal, Max Dowman ameendelea kuvunja rekodi moja baada ya nyingine na alikuwa mchezaji mdogo zaidi kucheza michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, mchezaji mdogo zaidi kuanza katika mechi ya Arsenal na mdogo zaidi kufunga goli katika historia ya Ligi Kuu England akiwa na umri wa miaka 16 na siku 73.
Dowman pia ni mchezaji wa pili mdogo zaidi kuichezea Arsenal na wa pili mdogo zaidi kucheza Ligi Kuu England, baada ya mwenzake kutoka kwenye akademia ya Arsenal, Ethan Nwaneri.
Dowman amekuwa akipata nafasi katika kikosi cha kwanza tangu akiwa na umri wa miaka 14 na kipaji chake kimepewa sifa kubwa na kocha wake, Mikel Arteta ambaye anamlinganisha na Lionel Messi.
Katika mechi hiyo dhidi ya Everton licha ya kupata wakati mgumu hasa kipindi cha kwanza ikikosa mabao, kipindi cha pili Arteta aliwaingiza Dowman na Viktor Gyokeres na kubadilisha mechi.
Bao la kwanza lilichangiwa na Dowman baada ya krosi yake kuleta madhara langoni mwa kipa Jordan Pickford aliyefanya makosa, kabla ya Gyokeres kuifungia Arsenal, kabla ya kinda huyo kufunga bao la pili akipokea pasi kutoka kwa Gabriel Martinelli.
Akizungumzia bao hilo la Dowman, Arteta alisema; “Ilikuwa ni tukio zuri sana, hasa jinsi lilivyotengenezwa, tulikuwa na sekunde 10-15 kufurahia. Hali hiyo ilikuwa kama ya kichawi. Hakika siyo tu goli ambalo amefunga, Dowman alibadilisha mchezo. Kila alipokuwa na mpira, alileta madhara. Kufanya hivyo akiwa na umri huu na presha ya ushindi, siyo kawaida.”
Kabla ya wababe hao kumalizana katika ligi, zitakutana wikiendi ijayo, Machi 22 katika fainali ya Kombe la Carabao.
ZILIZOBAKIA ARSENAL
11.04. 14:30
Arsenal v Bournemouth
19.04. 18:30
Manchester City v Arsenal
25.04. 19:30
Arsenal v Newcastle
02.05. 17:00
Arsenal v Fulham
09.05. 17:00
West Ham v Arsenal
17.05. 17:00
Arsenal v Burnley
24.05. 18:00
Crystal Palace v Arsenal
KWA CITY SASA
12.04. 18:30
Chelsea v Manchester City
19.04. 18:30
Manchester City v Arsenal
26.04. 16:00
Burnley v Manchester City
02.05. 17:00
Everton v Manchester City
09.05. 17:00
Manchester City v Brentford
17.05. 17:00
Bournemouth v Manchester City
24.05. 18:00
Manchester City v Aston Villa