David Alaba afanyiwa uchunguzi wa afya
Muktasari:
- Alaba alianzishwa kwa mara ya kwanza kwenye La Liga msimu huu kwenye mchezo huo dhidi ya Getafe, lakini alicheza kwa dakika 45, ambapo Raul Asencio aliingizwa baadala yake.
MADRID, HISPANIA: REAL Madrid itamfanyia uchunguzi wa kiafya beki wao wa kati, David Alaba baada kushindwa kumaliza Jumapili iliyopita alipotolewa wakati wa mapumziko dhidi ya Getafe.
Alaba alianzishwa kwa mara ya kwanza kwenye La Liga msimu huu kwenye mchezo huo dhidi ya Getafe, lakini alicheza kwa dakika 45, ambapo Raul Asencio aliingizwa baadala yake.
Kocha wa Los Blancos, Xabi Alonso amesema baada ya mechi kwamba Alaba alihisi maumivu kwenye kigimbi na hivyo ilitarajia kukufanyiwa uchunguzi zaidi Jumatatu kutambua ukubwa wa tatizo lake la majeraha.
"Kigimbi cha Alaba kilionekana kuwa na tatizo na hatukutaka apate matatizo zaidi. Tutamfanyia uchunguzi zaidi," amesema Alonso.
Alaba amecheza mechi tatu tu kwenye ligi msimu huu na hakuna uhakika mkubwa wa kuhusu hatima yake baada ya beki huyo mwenye umri wa miaka 33 mkataba wake kufika tamati mwishoni mwa msimu huu.
Real Madrid kwa sasa inawakosa mabeki wake kama Dean Huijsen, Antonio Rudiger, Trent Alexander-Arnold, Dani Carvajal na Ferland Mendy kutokana na kuwa majeruhi.
Hata hivyo, Mendy amerejea mazoezini, wakati Alexander-Arnold, Carvajal na Huijsen nao wanaweza kurudi uwanjani wakati Los Blancos itakapokipiga kwenye El Clasico.
Real Madrid ilipambana kupata pointi tatu dhidi ya Getafe, ambayo ilimaliza na wachezaji tisa.
Kylian Mbappe alifunga bao la ushindi kwenye dakika ya 80 na hivyo kuwarejesha Los Blancos kwenye kilele cha La Liga wakielekea wikiendi ya kukabiliana na Barcelona.
"Tunafurahia jinsi Kylian anavyofanya. Amekuwa akiamua kutokana na mambo yake pamoja na ushiriki wake. Mabao yanaleta pointi, lakini tunamhitaji kila mtu awe tayari."
Real Madrid itarudi uwanjani kusaka ushindi wa nne mfululizo itakapokipiga na Juventus uwanjani Bernabeu kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya, Jumatano usiku.