Conte awaondoa mashabiki hofu

LONDON, ENGLAND. KOCHA wa Tottenham, Antonio Conte amethibitisha upasuaji wa kibofu cha nyongo umefanyika salama lakini hatarejea katika majukumu yake ya ukocha hadi atakapopata nafuu.

Conte alifanyiwa upasuaji jana nyumbani kwao Italia baada ya kusumbuliwa na maumivu makali lakini bado haijafahamika atakuwa nje ya dimba kwa muda gani.
Tatizo hilo lilimtokea alipokuwa mapumziko pamoja na familia yake jijini Turin baada ya ushindi waliopata dhidi Preston kwenye michuano ya Kombe la FA.

Muitaliano huyo aliandika ujumbe mfupi kupitia akaunti yake ya Instram akiwashukuru mashabiki kutokana na maneno yao ya kumtia nguvu.

"Asanteni sana kwa meseji zenu, upasuaji umefanyika salama na najisikia vizuri sasa, naamini nitarudi haraka iwezekanavyo,"  aliandika Conte

Taarida zimeripoti Conte ataendelea kubaki Italia akiendelea na matibabu baada ya upasuaji huo halafu baadaye atarudi jijini London.

Kwasasa Tottenham itanolewa na kocha msaidizi Cristian Stellini na atakiongoza kikosi kuelekea mechi yao ya Ligi Kuu England dhidi ya Manchester City utakaochezwa kesho kutwa, kabla ya kumenyana na Leicester City.

Totteham itacheza mechi ugenini dhidi ya AC Milan kwenye mechi yao ya kwanza ya mtoano ya Ligi Mabingwa Ulaya raundi ya 16 bora, kabla ya mechi nyingine za ligi dhidi ya West Ham na Chelsea mwezi huu.