Bayern Munich yataja bei ya Olise
Muktasari:
- Olise ambaye hapo awali alidaiwa kuwa ana kipengele kinachoiruhusu timu inayomhitaji kutoa kiasi maalum cha pesa ili kuvunja mkataba wake, amekuwa akihitajika na vigogo wengi barani Ulaya kutokana na kiwango bora alichoonyesha tangu atue Bayern Munich mwaka jana
MUNICH, UJERUMANI: KIGOGO wa Bayern Munich Max Eberl, amesema timu yake itahitaji zaidi ya Euro 100 milioni ili kumuuza winga wao wa kimataifa wa Ufaransa, Michael Olise mwenye umri wa 23 ambaye Liverpool na Manchester City zimeonyesha nia ya kuitaka huduma yake.
Olise ambaye hapo awali alidaiwa kuwa ana kipengele kinachoiruhusu timu inayomhitaji kutoa kiasi maalum cha pesa ili kuvunja mkataba wake, amekuwa akihitajika na vigogo wengi barani Ulaya kutokana na kiwango bora alichoonyesha tangu atue Bayern Munich mwaka jana.
Eberl alidai wapo tayari kujadili na timu yoyote inayomhitaji Olise lakini ofa itakayowasilishwa itatakiwa kuanzia Euro 100 milioni na kuendelea.
Liverpool inamwangalia fundi huyu kama sehemu ya maboresho ya safu yao ya ushambuliaji ambayo imekuwa ikipiti changamoto nyingi tangu kuanza kwa msimu huu.
Mohamed Salah anaonekana kuwa na asilimia nyingi za kuondoka ifikapo mwisho wa msimu na Olise anaweza kuwa mbadala wake.
Mkataba wa sasa wa staa huyu unatarajiwa kumalizika mwaka 2029 na Bayern inaamini inaweza kupata hata mara mbili ya Euro 60 milioni ambazo ililipa mwaka jana kumsajili akitokea Crystal Palace.
Tangu kuanza kwa msimu huu, Olise amecheza mechi 17 za michuano yote, amefunga mabao tisa na kutoa asisti nane.