Bado sita tu kufuzu Kombe la Dunia 2026
Muktasari:
- Kuanzia Juni 11 hadi Julai 19, 2026, zitafanyika fainali hizo katika viwanja 16 vilivyo kwenye miji 16 tofauti, huku timu 48 kutoka mashirikisho sita ya soka duniani zikichuana kuwania ubingwa unaoshikiliwa na Argentina.
HADI kufikia leo Jumatano Novemba 19, 2025, tayari timu za mataifa 42 zimejihakikishia nafasi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwaka 2026 katika nchi za Canada, Mexico na Marekani.
Kuanzia Juni 11 hadi Julai 19, 2026, zitafanyika fainali hizo katika viwanja 16 vilivyo kwenye miji 16 tofauti, huku timu 48 kutoka mashirikisho sita ya soka duniani zikichuana kuwania ubingwa unaoshikiliwa na Argentina.
Katika mashirikisho hayo sita, lile la Ulaya ndiyo lina timu nyingi hadi sasa zikiwa zimefuzu 12, zitaongezeka zingine nne baada ya kumaliza mtoano. Inafuatiwa na Afrika yenye tisa, kisha Asia (8). Conmebol ambalo ni Amerika Kusini na Concacaf inayohusisha Amerika Kaskazini, Kati na Caribbean kila moja ina timu sita. Oceania ni moja pekee.
Ukiangalia timu 42 zilizofuzu hadi sasa, zipo nne ambazo zinakwenda kushiriki Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza. Timu hizo ni Jordan, Uzbekistan, Cape Verde na Curaçao.
Kwa Curaçao, linakuwa taifa dogo zaidi kuwahi kufuzu kwa Kombe la Dunia kwani lina idadi ya watu 155,000.
Wakati mataifa 42 yakifuzu kushiriki Kombe la Dunia 2026, kuna nafasi nne kutoka Ulaya ambapo zinakwenda kuchezwa mechi za mtoano zikihusisha mataifa 16.
Pia nafasi zingine zitapatikana kupitia mashindano ya mchujo ya mabara, huko ndipo DR Congo inasaka nafasi ya kwenda kushiriki Kombe la Dunia.
TIMU ZILIZOFUZU HADI SASA
OCEANIA: New Zealand
CONMEBOL: Argentina, Brazil, Ecuador, Uruguay, Paraguay, Colombia
CONCACAF: Canada (mwenyeji), Mexico (mwenyeji), Marekani (mwenyeji), Haiti, Panama, Curaçao
ASIA: Japan, Korea Kusini, Iran, Jordan, Australia, Qatar, Saudi Arabia, Uzbekistan
AFRIKA: Morocco, Tunisia, Misri, Algeria, Ghana, Cape Verde, Afrika Kusini, Ivory Coast, Senegal
ULAYA: England, Ufaransa, Croatia, Ureno, Norway, Uholanzi, Ujerumani, Hispania, Ubelgiji, Uswisi, Scotland, Austria