Ufaransa yaizima Senegal ikiifumua 3-1
Muktasari:
- Haikuwa rahisi kwa Ufaransa kupata ushindi huo, kwani kipindi cha kwanza imeshindwa kuufungua ukuta wa Senegal ambao ulikuwa bora kuzima mashambulizi.
Ufaransa imefanikiwa kulinda heshima yake, ikipata ushindi wa mabao 3-1 mbele ya Senegal ulioifanya kuanza vizuri fainali za Kombe la Dunia 2026.
Haikuwa rahisi kwa Ufaransa kupata ushindi huo, kwani kipindi cha kwanza imeshindwa kuufungua ukuta wa Senegal ambao ulikuwa bora kuzima mashambulizi.
Ufaransa imelazimika kusubiri mpaka dakika ya 66 kupata bao la kwanza lililofungwa na mshambuliaji na nahodha wa timu hiyo, Kylan Mbappe aliyetengenezewa asisti na kiungo Michael Olise.
Dakika moja baadaye Nikolas Jackson amefunga bao kwa shuti kali, lakini likakataliwa baada ya kunaswa akiwa ameotea wakati anapokea pasi ya mwisho.
Dakika ya 80 Ufaransa ikafanya mabadiliko ya kiufundi ikimtoa winga wake Ousmane Dembele na nafasi yake ikachukuliwa na Bradley Barcola.
Mabadiliko hayo yakaipa Ufaransa bao la pili mfungaji akiwa Barcola, akimfunga kiufundi kipa wa Senegal, Eduardo Mendy, akitumia asisti ya Adrien Rabiot.
Ibrahim Mbaye aliyeingia kipindi cha pili akairudisha mchezoni Senegal akifunga bao zuri kwa shuti kali dakika ya 90+5 na kufanya matokeo kusomeka 2-1.
Lakini wakati Senegal wakishangilia, Mbappe tmakaipa bao la tatu Ufaransa dakika ya 90+6 kwa shuti kali la mbali akipokea asisti ya Olise.
Mabao hayo mawili ya Mbappe yanamfanya kufikisha jumla 14 aliyofunga katika fainali tatu za Kombe la Dunia.