Arsenal yaendeleza ubabe

LONDON, ENGLAND. Baada ya upepo mbaya kuwapitia, mashabiki wa Arsenal wameanza kushusha pumzi katika siku za hivi karibuni baada ya timu yao kuibuka na ushindi katika mechi mbili mfululizo za Ligi Kuu England.
Arsenal ilipata ushindi wa bao 1-0 leo dhidi ya Burnley baada ya wiki iliyopita kutoa gundu kwa kuibamiza Norwich bao 1-0.
Kabla ya ushindi wa mechi hizo mbili Arsenal haikuwahi kupata ushindi wowote tangu ilipoanza ligi ambapo ilianza kufungwa na Brentford, Chelsea Kabla ya kupata kipigo cha aibu cha mabao 5-0 kutoka kwa Man City.
Ushindi wa leo umeifanya timu hiyo kufikisha alama sita ambazo zimeipandisha hadi nafasi ya 12.
Mbali ya mechi hiyo, mechi ya mapema nchini humo ilizikutanisha Wolves dhidi ya Brentford iliyoibuka na ushindi wa mabao 2-0 licha ya mchezaji wao kutolewa kwa kadi nyekundu.
Liverpool pia ikashinda mabao 3-0 dhidi ya Crstal Palace yaliyofungwa na Sadio Mane, Mohamed Salah na Naby Keita.
Man City iliyokuwa kwenye dimba lake la nyumbani ilibanwa mbavu na kutoka sare ya 0-0 na Southampton wakati Watford ikiibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Norwich City.