Aliyekuwa mlinzi wa Ronaldo afunguka

Muktasari:
- Hichman, ambaye ni PMC (Private Military Contractor) na CPO (Close Protection Operative), ana zaidi ya wafuasi 127,000 kwenye ukurasa wake wa Instagram na alifanya kazi ya kumlinda Ronaldo na familia yake kwa kipindi cha miaka minne.
RIYADH, SAUDI ARABIA: MLINZI wa zamani wa Cristiano Ronaldo, Hichman Bukhari, amefichua jinsi ilivyokuwa akifanya kazi ya kumlinda nyota huyo wa zamani wa Manchester United na Real Madrid katika maisha ya kila siku.
Hichman, ambaye ni PMC (Private Military Contractor) na CPO (Close Protection Operative), ana zaidi ya wafuasi 127,000 kwenye ukurasa wake wa Instagram na alifanya kazi ya kumlinda Ronaldo na familia yake kwa kipindi cha miaka minne.
Alipokuwa akifanya kazi hiyo jijini Madrid, Bukhari anakumbuka changamoto nyingi walizokumbana nazo kwa lengo la kuhakikisha usalama wa Ronaldo, mpenzi wake Georgina Rodriguez, na watoto wao.
“Lazima kila mara tujue tunakoenda, nani atakuwepo, na tujue njia rahisi za kuingia na kutoka pamoja na maeneo ya mawasiliano. Ni lazima tufahamu kuwa maisha yetu yanaweza kuwa hatarini. Lazima tuwe tayari kulinda mtu, na wakati mwingine kujitoa mhanga kwa ajili yao. Kama nitahitaji kutumia silaha, nitazitumia. Jambo la msingi ni kuwa na uwezo wa kufikiri haraka, kutatua matatizo, na kubaki mtulivu katika hali ngumu.”
Ingawa Ronaldo hakuwa mlengwa wa hatari ya juu kama watu waliotishiwa kuuawa au kutekwa, Bukhari anasema aliwahi kutishiwa na mashabiki na watu waliotaka kumwibia staa huyo.
Hichman anadai alipokea Pauni 850 kwa siku alipokuwa akimhudumia mshindi mara tano huyo wa Ballon d’Or. Kuhusu uhusiano wake na Ronaldo, alisema: “Yeye ndiye bosi bora kabisa niliyewahi kufanya naye kazi. Tuna uhusiano mzuri sana. Haikuwa kama kumlinda mtu aliyekuwa katika hatari ya kuuawa au kutekwa. Tulikuwa na matukio madogo tu kama ya wapiga picha au mashabiki waliopitiliza mipaka, lakini hakuna tukio kubwa. Ni mtu mzuri sana, mkarimu, si kama watu wanavyomchukulia.”
Mwaka 2023, ilifichuka kuwa mmoja wa walinzi wa Ronaldo alikuwa bondia wa zamani wa MMA, Goncalo Salgado, ambaye alihamia kwenye kazi ya ulinzi binafsi baada ya kustaafu.
Pia, Ronaldo aliimarisha ulinzi wake alipojiunga tena na Manchester United kwa kuwaajiri mapacha Sergio na Jorge Ramalheiro, ambao waliwahi kutumikia jeshi la Ureno katika kikosi maalum kilichopambana nchini Afghanistan.
Mapacha hao wawili waliwahi kulinda viongozi wa kisiasa kabla ya kuchukua likizo bila malipo ili kumlinda Ronaldo.
Mapacha hao pia walionekana katika utambulisho rasmi wa Ronaldo kama mchezaji wa Al Nassr mwaka 2023.