Neville awajia juu mabosi OT

MANCHESTER ENGLAND. BEKI wa zamani wa Manchester United, Gary Neville amewaponda mabosi wa klabu hiyo kuwa bado wameendelea kuzingua kwenye ishu za usajili miaka yote.
Licha ya Man United kusajili wachezaji watatu wapya (Lisandro Martinez, Tyrell Malacia, Christian Eriksen) Neville bado anaamini, timu hiyo inahitaji kuboresha maeneo mengine.
Neville amechukizwa na mwenendo mbovu wa usajili hususan ishu ya Frankie de Jong, kwani mwafaka bado haujapatikana licha ya kufikia makubaliano ya uhamisho na Barcelona.
Aidha mkongwe huyo bado haamini kama Erik ten Hag amepewa sapoti ya kutosha na Bodi ya Man United kwenye ishu za usajili tangu alipoanza kufanya kazi akitokea Ajax.
Akizungumza kupitia Mtandao wa Overlap, Neville amesema: “Nitaenda kwa Ten Hag na kumpa pongezi kwa alichokifanya, nadhani amefanya kazi nzuri, ameanza vizuri kwa upande wangu, lakini bado hajapewa sapoti ya kutosha na bodi, hajapata wachezaji wake anaowahitaji, wanampa wakati mgumu sana kocha.
“Man City imemsajili Erling Haaland, Chelsea imenasa Raheem Sterling, Darwin Nunez ameelekea Liverpool, utaona kabisa klabu hizi zimefanya usajili mzuri sana, lakini kwa upande wetu hatupati wachezaji tunaowahitaji,” aliongeza Neville.
Licha ya Neville kuitolea povu, Man United imeanza mazungumzo na RB Salzburg, kwaajili ya straika wao, Benjamin Sesko mwenye thamani ya Pauni 55 milioni. Hata hivyo Chelsea imeingia katika kinyang’anyiro cha kuwania saini ya kinda huyo mwenye umri wa miaka 19.