Achraf Hakimi ampiga chenga ya mwili mkewe
PARIS, UFARANSA. Mchezaji wa kimataifa wa Morocco, Achraf Hakimi amekuwa na mada inayovuma duniani kote baada ya mke wake kugundua kuwa hamiliki chochote licha ya kupokea mamilioni ya pesa kutoka kwa klabu ya Paris Saint- Germain na timu ya taifa ya soka ya Morocco.
Ugunduzi huu ulifanywa wakati wa kesi ya talaka inayoendelea mahakamani baada ya mkewe, Hiba Abouk, kuwasilisha talaka Machi 2023 mwaka huu na kuomba apewe nusu ya mali na pesa zote alizomiliki mwanasoka huyo.
Kwa kushangaza aligundua kuwa Hakimi aliandika jina la mama yake mzazi kwenye Mali zake zote, hiyo inamaanisha kwamba kila alipohitaji chochote, alikuwa akimwomba mama yake amnunulie.
Nyumba zake zote, magari, nguo, na vito vyake vyote vilipatikana kwa jina la mama yake, ikiwemo mamilioni ya mshahara anayolipwa kutokana na kazi yake.
Iliripotiwa kuwa asilimia 80 ya vitu vyote alivyo navyo imesajiliwa kwa jina la mamake.
Wanandoa hao walianza kuchumbiana mwakan2018 na kufunga pingu za maisha mwaka 2020 na wakabahatika kupata watoto wawili wa kiume.
Hakimi anayechunguzwa huko Paris, Ufaransa, kwa madai ya ubakaji, ndoa yake na mwigizaji huyo wa Kihispania ilikuwa tayari imeingia dosari baada ya kesi hiyo inayomkabili.
Hatua ya Hakimi kutosajili utajiri wake kwa jina lake imekuwa habari kubwa kwenye mitandao ya kijamii, huku wengine wakimsifu na kumponda.