Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Posta Rangers yaiadhibu Shabana, yakaa kileleni kibabe

Muktasari:

  • Brian Marita aliipa Posta uongozi mwishoni mwa kipindi cha kwanza, kabla ya Shabana kukosa penalti muhimu katika dakika ya 65. Dakika 12 baadaye, Posta waliongeza bao la pili katika dakika ya 77.

Shabana FC imepoteza mechi yake ya kwanza ya msimu huu kwenye Ligi Kuu ya Soka ya Kenya (FKF Premier League) baada ya kuchapwa mabao 2–1 nyumbani na Posta Rangers, leo Oktoba 15, 2025.

Brian Marita aliipa Posta uongozi mwishoni mwa kipindi cha kwanza, kabla ya Shabana kukosa penalti muhimu katika dakika ya 65. Dakika 12 baadaye, Posta waliongeza bao la pili katika dakika ya 77.

Kikosi cha Shabana, kinachotoka eneo la Gusii, kilipata bao la kufutia machozi dakika za mwisho, huku Posta Rangers ikikaa imara na kuondoka na ushindi muhimu uliowapandisha kileleni mwa msimamo ikiwa na pointi 10.

Shabana iliingia uwanjani ikiwa na matumaini ya kurejea kwenye njia ya ushindi baada ya kutoka sare ya 1-1 dhidi ya Tusker kwenye mechi iliyopita na bahati mbaya ikakutana na kichapo cha kwanza msimu huu wakati Posta ikibaki timu isiyopoteza msimu huu sambamba na Kenya Police na AFC Leopards kati ya timu 18 zinazoshiriki ligi hiyo iliyoingia raundi ya nne.


KAKAMEGA 3-1 BIDCO
Kakamega Homeboyz imerejea katika njia ya ushindi kwa kishindo baada ya kuilaza Bidco United mabao 3-1, mechi ikichezwa uwanja wa Bukhungu.

Mabao ya Henry Omollo, bao la kujifunga la Kevin Ouma, na shuti kali la mwisho kutoka kwa Oliver Majaka yaliihakikishia Homeboyz ushindi wa kuvutia, baada ya Bidco kutangulia kufunga kupitia kwa Dennis Murunga.

Matokeo hayo yalipelekea Bidco kupata kichapo chao cha kwanza msimu huu, huku kikosi cha kocha Patrick Odhiambo kikisherehekea ushindi wao wa pili wa msimu.

Kwa timu zote mbili zikiwa na malengo tofauti, Homeboyz ikitaka kufufua matumaini na Bidco ikilenga ushindi wa tatu mfululizo, mchezo ulianza kwa kasi ya juu.

Homeboyz ilikuwa ya kwanza kuliandama lango la Bidco kupitia Omollo ambaye alipiga shuti dhaifu lililodakwa na kipa Issa Emuria. Dakika chache baadaye, Samuel Odaro alikimbia kwa kasi upande wa kulia lakini Emuria alizuia tena kwa ustadi.

Bidco ilijibu kupitia John Kelwish, ambaye shuti lake la chini kutoka kwa krosi ya Thomas Wainaina liliokolewa na Potiphar Odhiambo.

Katikati ya kipindi cha kwanza, Josphat Lopaga alipoteza nafasi nzuri baada ya kupiga juu ya lango, kabla ya Kelwish kukosa bao kwa inchi chache tu.

Dakika ya 30, Bidco ilipata bao la kuongoza kupitia Dennis Murunga, aliyemalizia kwa ustadi pasi safi ya Idriss kwa “backheel” ya kuvutia.

Hata hivyo, Homeboyz haikusubiri muda mrefu kujibu. Dakika tatu baadaye, Henry Omollo, aliyewahi kuchezea Bidco, aliisawazishia Homeboyz kwa shuti kali lililompiga chenga kipa Emuria.

Kabla ya mapumziko, Masava alipiga shuti lililogonga mwamba, huku Lopaga na Hillary Otieno wakikosa nafasi chache muhimu, na hivyo kipindi cha kwanza kumalizika 1-1.

Baada ya mapumziko, Homeboyz ilionekana bora zaidi, ikicheza kwa kasi na kuishinikiza Bidco katika eneo lao. Dakika ya 55, Omollo alikaribia kufunga bao la pili lakini kipa Emuria alifanya kazi nzuri kuokoa.

Bidco ilijaribu kujibu kupitia mchezaji wa akiba Clinton Asiago, lakini alipoteza nafasi nzuri baada ya kushindwa kuunganisha krosi ya Herman Ngala.

Dakika ya 64, Homeboyz ilipata bao la pili baada ya krosi kali ya John Omondi kumfanya Kevin Ouma kujifunga kwa bahati mbaya, na kuipa Homeboyz uongozi wa 2-1.

Mabadiliko ya kocha Odhiambo yalizaa matunda, kwani mchezaji wa akiba, Oliver Majaka aliingia na kuleta tofauti kubwa. Dakika ya 78, shuti lake la kwanza liliokolewa na kipa Emuria, huku jaribio la Nyatini likizuiwa kwenye mstari.

Bidco ilijaribu kusawazisha dakika za mwisho, lakini Homeboyz ilizika matumaini yao dakika za mwisho, wakati Majaka alipofunga bao zuri la tatu baada ya kupokea pasi nzuri ya Derrick Otanga.

Ushindi huo umewarudishia morali wachezaji wa Kakamega Homeboyz baada ya kichapo cha wiki iliyopita dhidi ya Nairobi United, huku ukisitisha rekodi ya Bidco ya kutopoteza tangu kuanza kwa msimu.

Katika matokeo mengine ya mechi za leo Jumatano Oktoba 15, 2025, Sofapaka imeitandika Murang'a SEAL mabao 2-1, huku AFC Leopards na Bandari zikishindwa kufungana.