GOR MAHIA YAMWACHA KIPA WAO KWA MATAA
KIPA wa zamani wa Harambee Stars Boniface Oluoch kaachwa kwa mataa na klabu yake Gor Mahia kuhusiana na ile faini aliyopigwa na CAF.
Mei mwaka huu Oluoch na kiungo wa zamani wa Gor Kenneth Muguna walipigwa faini ya Sh1.5 milioni kila mmoja.
Hii ilikuwa ni baada ya wawili hao kupatikana na makosa ya kumshambulia refa aliyechezesha mechi kati ya Gor na Napsa Stars wa Zambia mnamo Februari 2021, ambako Gor walibanduliwa nje ya dimba hilo la CAF Confederation Cup.
Akizungumzia ishu hiyo, mwenyekiti wa Gor Ambrose Rachier alimruka Oluoch kwa kusema kuwa faini aliyopigwa ni mzigo wa kibinfasi na wala sio wa klabu.
Kulingana na Rachier, mzigo pekee walioyokuwa nayo kama klabu ni zile faini za wachezaji wao wa zamani waliowavunjia mikataba yao bila kufuata utaratibu na wakaishia kuwashtaki kwa FIFA.
"Tushamalizana na madeni yote ya wachezaji wetu wa zamani na FIFA tayari imeshatuondolea marufuku ya kutofanya usajili iliyokuwa umetuwekea. Kuhusu zile faini walizopokea wachezaji, zile hazikuwa faini zetu, zile ni faini za kibinfasi." Rachier alimruka Oluoch.
Hali hiyo sasa imemwacha pabaya Oluoch ambaye pia pale Gor alishapoteza namba toka ujio wa Gad Mathews.
Tayari benchi la ukufunzi limeonyesha nia ya kumtema Oluoch kabla ya kuanza kwa msimu mpya.
Kwa upande wa mwenzake Muguna, kiungo huyo alitumia fedha alizolipwa kama Sign On Fee na Azam baada ya kujiunga nao.
"Sio kwamba Azam ilimlipia faini yake Muguna kama jinsi ilivyoripotiwa. Alichofanya Muguna ni kutumia sehemu ya fedha alizolipwa kama Sign-on fee kumalizana na CAF. Boniface nimemwita nimsaidie kuiandikia CAF barua kuwa imruhusu kulipa fedha hizo mdogo mdogo ila jamaa ni kama hajiskii." kasema Mkurugenzi wa Gor Lordvic Aduda.