Gor Mahia yamuenzi Raila Odinga kwa ushindi mnono
Muktasari:
- Mechi hiyo ilianza kwa dakika moja ya ukimya kumuenzi aliyekuwa Waziri Mkuu wa zamani wa Kenya, Raila Odinga, aliyefariki Oktoba 15, 2025 akiwa na umri wa miaka 80.
Gor Mahia imeichapa Posta Rangers mabao 3-0 kupitia Ben Stanley, Austin Odhiambo, na Felix Oluoch.
Mechi hiyo ilianza kwa dakika moja ya ukimya kumuenzi aliyekuwa Waziri Mkuu wa zamani wa Kenya, Raila Odinga, aliyefariki Oktoba 15, 2025 akiwa na umri wa miaka 80.
Odinga alikuwa mfadhili na mlezi mkuu wa Gor Mahia, na hii ilikuwa mechi ya kwanza kwa timu hiyo tangu kifo chake. Mashabiki wa K’Ogalo walibeba mabango yenye picha yake, na dakika ya 80 waliimba kwa sauti “Jowi! Jowi!” wakimsherehekea kwa dakika moja ya makofi.
Baada ya mechi, kocha wa Gor Mahia, Charles Akonnor alisema timu ilikuwa chini ya shinikizo la lazima kushinda ili kumheshimu marehemu Odinga.
“Mchezo huu ulikuwa kwa ajili ya Raila Odinga,” amesema Akonnor.
Kocha huyo Mghana amesema mabadiliko waliyofanya kipindi cha pili yalibadili mchezo.
“Posta Rangers ni timu nzuri. Walitufanya kipindi cha kwanza kiwe kigumu, lakini matokeo yanaonyesha jinsi tulivyo na mbinu. Kabla ya mchezo tuliamini wachezaji wa benchi wangeleta tofauti, na tuliwaandaa kisaikolojia kwa kazi hiyo,” ameongeza.
Kwa upande wake, kocha wa Posta Rangers, Sammy ‘Pamzo’ Omollo amesema timu yake ilijiharibia wenyewe.
“Tulifanikiwa kuwadhibiti Gor kipindi cha kwanza, lakini kipindi cha pili tulifanya makosa ambayo huwezi kuyafanya dhidi ya timu kama Gor Mahia. Tunapaswa kujirekebisha,” amesema Pamzo.
Kipindi cha kwanza hakikuwa na nafasi nyingi za wazi, huku Kevin Juma wa Posta Rangers akikosa nafasi nzuri dakika ya 41 baada ya kipa Byrne Omondi wa Gor Mahia kuokoa shuti kali.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi zaidi baada ya makocha wote kufanya mabadiliko. Akonnor alimtoa Samuel Kapen na kumuingiza Alpha Onyango, ambaye aliongeza kasi ya mchezo.
Uchezaji wa winga Sherif Musa ulitishia ngome ya Posta Rangers dakika ya 54 alipowachanganya mabeki na kutoa krosi ya chini iliyopigwa juu ya lango na Fidel Origa.
Dakika nne baadaye, Origa na Patrice Esombe walitolewa, wakapishwa na Ben Stanley Omondi na Felix Oluoch.
Mara tu baada ya kuingia, Ben Stanley aliipatia Gor Mahia bao la kwanza kwa kichwa baada ya kupokea krosi ya Musa na hapo ndipo mchezo ukageuka kabisa kwa faida ya K’Ogalo.