Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Ambani aendeleza rekodi bora, Leopards ikitakata Mashemeji Derby

Muktasari:

  • Ingawa Gor Mahia ilikuwa mwenyeji wa mechi hiyo, lakini Leopards ikiongozwa na Ambani, upande wao ndiyo ulikuwa ukisherehekea ushindi na kujivunia ubabe, kufuatia bao la Julius Masaba dakika ya 25 ambalo liliwapa ushindi huo.

Kocha wa AFC Leopards, Fred Ambani, ameendeleza rekodi yake ya kutopoteza dhidi ya Gor Mahia baada ya kuiongoza timu hiyo kushinda katika Dabi ya 98 ya Mashemeji kwenye Uwanja wa Nyayo, jana Jumapili Desemba 7, 2025.

Ingawa Gor Mahia ilikuwa mwenyeji wa mechi hiyo, lakini Leopards ikiongozwa na Ambani, upande wao ndiyo ulikuwa ukisherehekea ushindi na kujivunia ubabe, kufuatia bao la Julius Masaba dakika ya 25 ambalo liliwapa ushindi huo.

Mechi hiyo iliakisi ubora uliotarajiwa, ikijaa mbinu na kukabiliana kwa nguvu kutoka pande zote mbili, lakini Leopards iliibuka na ushindi huku Gor Mahia ikizimwa.

Gor Mahia ilipata nafasi ya kwanza pale Shariff Musa alipounganisha krosi nzuri baada ya kona, lakini shuti lake mpira ulimgonga Randi Bakari na kutoka nje.

Hiyo ilikuwa dakika ya 21, na dakika nne baadaye, Ingwe walishangilia bao pekee kufuatia kujipanga kwao vizuri na kupigiana pasi katika upande wa kulia wa ushambuliaji wa Leopards, ikamfikia Tyson Otieno akiwa na nafasi nje ya boksi. Kiungo huyo wa zamani wa Kenya Police alikandamiza shuti kali, kipa wa Gor Mahia Byrne Omondi akalipangua, lakini mpira uliangukia kwa Masaba aliyekuwa hana ulinzi na akatupia kimiani kirahisi kabisa.

Leopards ilipaswa kuongeza bao la pili dakika za mwisho za kipindi cha kwanza baada ya James Kinyanjui kupiga krosi tamu, lakini Victor Omune alishindwa kuunganisha akiwa kwenye nafasi nzuri.

Hakikuwa kipindi cha kwanza kizuri kwa Gor Mahia, ambayo haikupiga shuti hata moja lililolenga lango, huku Leopards ikipiga mawili.

Baada ya mapumziko, Leopards iliwaumiza zaidi wapinzani kwa kucheza kwa kujilinda chini, na kuilazimu Gor Mahia kupiga mashuti ya mbali, kwanza kupitia Austin Odhiambo, kisha lingine kutoka kwa Musa.

Zaidi ya saa moja ya mechi kukamilika, Ambani aliamua kufanya mabadiliko ya kujilinda ili kulinda uongozi, akimtoa Omune na kumuingiza Ken Owino, lakini Leopards haikuwa kwenye hatari kubwa kutokana na Gor Mahia iliyokuwa chini ya kiwango.

Musa alipata nafasi ya dhahabu kusawazisha katika muda wa nyongeza, lakini shuti lake zuri likapaa juu ya lango la Humphrey Katasi.

Ingwe ilibaki imara hadi mwisho na kukusanya pointi zote tatu zinazowaweka nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Kenya ikiwa na pointi 17 kutokana na mechi 10, pointi mbili tu nyuma ya Gor Mahia, ambayo sasa imepoteza mechi mbili mfululizo.