Akumu ametoka Kisumu Allstars

Akumu ametoka Kisumu Allstars

NAIROBI. BEKI Vitalis Akumu amevunja ndoa yake na Kisumu All Stars ikiwa ni miezi michache baada ya kujiunga na klabu hiyo ambayo hushiriki mechi za Betika Supa Ligi ya Taifa (BNSL).

“Kamwe sio duru tena ila ni ukweli tumefikia makubaliano nikome kuichezea na kwa sasa ninasaka matunda mazuri kwingine. Tayari nimepokea ofa kadhaa kutoka klabu za Ligi Kuu ya Shirikisho la Soka la Kenya (FKF-PL),’’ amesema na kuongoza atafichua baadaye atakoelekea.

Mchana nyavu huyo ameitakia Kisumu Allstars mema kwenye kampeni za kufukuzia tiketi ya kufuzu kupandishwa ngazi kushiriki ligi kuu msimu ujao.

Hata hivyo Vihiga Bullets miongoni mwa vikosi vinavyotajwa kuwa vinawinda saini ya mchezaji huyo wa zamani wa Sofapaka FC maarufu Batoto ba Mungu.

Kando na Sofapaka beki huyo pia anajivunia kusakatia Western Stima iliyokuwa ikishiriki kipute cha FKF-PL kabla ya kushushwa daraja na kubandilisha jina ambapo inafahamika kama Kisumu United.

Kwa mara nyingine alishiriki mechi za ligi kuu akichezea Vihiga United kabla ya kuteremshwa ngazi.

Kipindi cha dirisha ndogo la uhamisho kilifunguliwa juzi Jumanne ambapo klabu nyingi zimo mbioni kusaka sajili wapya ili kujiongezea nguvu tayari kukabili wapinzani wao.