Zoran ampika Banda mpya

Zoran ampika Banda mpya

WINGA wa Simba, Peter Banda msimu uliopita hakuwa kwenye kiwango bora pengine kutokana na sababu ya ugeni wa ligi na kushindwa kupata nafasi ya kucheza kwenye kikosi mara kwa mara.

Banda alifanya mahojiano maalumu ya muda mfupi na Mwanaspoti hapa Ismailia Misri na kueleza sababu ya kwanza ni ugeni wa ligi ilikuwa shida kubwa kwake.

Alisema wakati Simba inamsajili ilimchukua kutokea Ulaya alikuwa amezoea mazingira ya huko ikiwemo hali ya hewa na aina ya uchezaji soka ambayo ni tofauti na Tanzania.

“Kiukweli nilikuwa napata shida nyingi mazingira ya viwanja, hali ya hewa, vyakula na aina ya mpira wa Tanzania ni tofauti na nilipotokea ila baada ya kukaa Simba kwa msimu mmoja nimezoea hivyo vyote na si changamoto tena kwangu,” alisema Banda na kuongeza;

“Hata wakati naenda kucheza soka kwa mara ya kwanza Ulaya nilipata wakati mgumu ila baada ya kuzoea nilicheza kwenye kiwango bora pengine hadi Simba kuvutiwa na uwezo wangu,”

“Bahati nzuri Mwanaspoti mmepata nafasi ya kushuhudia maandalizi yetu huko Misri nadhani unaona kwa kiasi kikubwa ambavyo nimeimarika zaidi ya msimu uliopita.

“Katika mazoezi yetu kocha amekuwa akinifuatilia zaidi nadhani anaamini nipo na kitu bora naweza kukionyesha ndio maana kuna wakati nikipatia kufanya vile ambavyo anataka amekuwa akinipongeza.”

Katika mazoezi hayo ya Simba kocha, Zoran Maki muda mwingi alikuwa akimuita muita Banda katika kila zoezi ambalo analitoa na kumtaka afanye zaidi kama ni kukimbia, kucheza mpira, kuruka koni au lingine lolote.

Banda alisema yale ya msimu uliopita yamekwisha na anaamini msimu ujao utakuwa bora kwao.