Simba, Yanga kazi ipo

Simba, Yanga kazi ipo

RATIBA ya Ligi Kuu Bara imetoka huku watani wa jadi wakipangwa kumalizana kwenye mechi ya raundi ya kwanza Jumapili, Oktoba 23, lakini kwenye michezo ya awali Simba na Azam zitaanzia nyumbani, huku Yanga ikipangwa kuanzia ugenini.

Akitangaza jana ratiba hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi (TPLB), Almasi Kasongo alisema ligi itazinduliwa na Ngao ya Jamii, Agosti 13 kisha ngwe kuanza siku mbili baadae kwa mechi kati ya

Ihefu na Ruvu Shooting na ile ya Namungo dhidi ya Mtibwa Sugar.

Simba yenyewe itakuwa wenyeji wa Geita Gold Agosti 17, siku ambayo pia kutakuwa na mechi nyingine ikiwamo ya Azam dhidi ya Kagera Sugar na Coastal Union itakayoialika KMC, jijini Tanga, lakini wageni Singida Big Stars watakata utepe Agosti 16 dhidi ya Tanzania Prisons mjini Singida siku ambayo Yanga itavaana na Polisi mjini Moshi na Dodoma Jiji itacheza na Mbeya Ciy.

Kasongo alisema ligi hiyo itaisha Mei 27, huku akisisitiza ratiba imezingatia mambo kadhaa ikiwamo kalenda ya CAF na Fifa, sambamba na Kombe la Azam Sports Federation Cup (ASFC) na ile ya Mapinduzi ambayo hufanyika Januari.

“Wakati wa Kombe la Dunia ligi yetu itaendelea kwa sababu hakuna timu inayotoa wachezaji kuanzia watatu kwa mujibu wa kanuni,” alisema.

Pambano la watani litapigwa katika raundi ya nane kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa kuanzia saa 11 jioni, huku kukiwa na kumbukumbu ya msimu uliopita timu hizo kushindwa kutambiana kwa kutoka suluhu kwenye mechi zote mbili.

Hilo litakuwa pambano la 109 kwa timu hizo kukutana kwenye Ligi ya Bara tangu mwaka 1965, huku rekodi zikionyesha kuwa, mara ya mwisho kwa Simba kupata ushindi mbele ya Yanga ni

Feb 16, 2019 pale Meddie Kagere aliyetemwa kwenye usajili ya msimu huu alipofunga bao pekee.