Yanga yazuia mashabiki mazoezini

Mashabiki wa Yanga zaidi ya 100 wamejikuta wakiishia getini kwenye uwanja wa Ilulu Lindi baada ya timu hiyo kuzuia mtu yoyote kuingia uwanjani kutazama mazoezi.

Mashabiki wengi walianza kufika uwanjani kuanzia Saa 9 Alasairi baada ya kusikia msafara wa timu utawasili Saa 10 kwa ajili ya mazoezi.

Hata hivyo licha ya basi la timu kufika Saa 10 jioni, makomandoo wa timu hiyo pamoja na Askari polisi waliimarisha ulinzi Ili kuhakikisha hakuna shabiki anayepita na kuingia ndani.

Polisi walifanya kazi ya ziada kuwataka mashabiki kusogea mbali na geti Ili kurubusu basi la timu kuingia ndani na mashabiki hao hawakubisha bali walirudi nyuma kama hatua tatu huku wakisikika wakisema hawasogei zaidi ya hapo.

Basi la wachezaji lilipowasili liliingia ndani likifuatiwa na gari nyeusi ya msemaji wa klabu hiyo, Haji Manara Kisha geti likafungwa haraka.

Hata waandishi wa habari waliokuwepo nje ya Uwanja huo wamezuiwa kuingia ndani kwa makomandoo kudai uongozi umekata yoyote kuingia kitazama Mazoezi.

Mmoja wa mashabiki waliofika uwanjani hapo, Fikirini Kassim amesema amepata hasira kuona amekodi pikipiki kuja kuangalia timu yake lakini amezuiwa.

"Timu yetu wenyewe lakini tunazuiwa jamani, wengine hela ya kiingilio kesho hatuna basi wangetuacha hata tumuone live kidogo Mayele turizike basi" amesema Kassim.

Shabiki mwingime alisikika akisema "Jamani Polisi wameshasema tuondoke, basi tuondoke yasije yakatokea kama ya Jana Mwanza kwa Simba mabomu yakapigwa, hata mimi ndio naondoka, bado napenda kuishi" alisema Shabiki huyo na kuwaacha watu wakiangua vicheko.