Yanga yamng'oa Mkurugenzi mmoja
Uongozi wa Yanga umemng'oa kwenye nafasi yake aliyekuwa Mkurugenzi wao wa mambo ya wanachama na mashabiki, Haji Mfikirwa, Mwanaspoti linafahamu.
Mfikirwa ajira yake hiyo imekoma rasmi jana Desemba 27 baada ya kutaarifiwa kuondolewa kwenye nafasi yake kufuatia kile kilichoelezwa kutofautiana na uongozi wa klabu hiyo juu ya utekelezaji wa majukumu yake.
Inaelezwa kwamba awali Yanga ilitangulia kumsimamisha Mfikirwa kabla ya kuchukua uamuzi wa kumuondoa Moja kwa moja kwenye nafasi hiyo.
Ingawa hakuna kiongozi wa Yanga aliyekuwa tayari kuelezea hilo kwa undani lakini Mwanaspoti linafahamu kuwa tayari uongozi wa klabu hiyo umeshawajulisha wakuu wa idara zote kuwa Mfikirwa ameondolewa ndani ya klabu hiyo.
"Nikweli Haji ameshaondolewa na hata kwenye mifumo yetu ya mawasiliano ya ndani ameshaondolewa, Kuna mambo yakitokea kwahiyo ameshaondoka Yanga,"amesema mmoja wa vigogo wa klabu hiyo.
Awali Mfikirwa kabla ya kupewa nafasi ya kuwa Mkurugenzi wa wanachama na mashabiki alitangulia kuwa Mkurugenzi wa Fedha kabla ya kuhamishiwa idara nyingine kufuatia mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji wa kisasa uliofanyika klabuni hapo.