Simba wamweka pabaya Pitso Mosimane Ahly

Muktasari:

Mosimane ameiongoza Al Ahly katika michezo 26 ambapo imeibuka na ushindi mara 20, kutoka sare nne na kufungwa michezo miwili

Kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Simba, Jumanne iliyopita kimemuweka katika wakati mgumu kocha wa Al Ahly, Pitso Mosimane ndani ya klabu hiyo kikionekana kutouridhisha uongozi wa timu hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa vyombo mbalimbali vya habari nchini humo, uongozi wa Ahly chini ya Rais wao, ulimweka kitimoto kocha huyo muda mfupi baada ya msafara wao kurejea Misri ukimhoji sababu hasa za kilichopelekea wapoteze mechi hiyo muhimu.

Katika kikao hicho kilichoongozwa na Rais wa Al Ahly, Mahmoud El-Khatib, Pitso alitakiwa kuwasilisha ripoti ya mechi hiyo ikiambatana na sababu za kiufundi zilizopelekea wapoteze mchezo lakini pia wakajadili maendeleo ya timu chini yake tangu alipojiunga nayo Oktoba 2020.

Kikao hicho cha uongozi wa Al Ahly kimekuja katika kipindi ambacho Mosimane amekuwa akipokea mashambulizi kutoka kwa baadhi ya mashabiki na wachezaji wa zamani wa timu hiyo wakidai makosa yake ndio yalikuwa chanzo cha timu yao kupoteza dhidi ya Simba.

Beki wa zamani wa Al Ahly, Wael Gomaa alisema kuwa Mosimane alichangia kwa kiasi kikubwa wao kupoteza mechi kutokana na maamuzi yake.

"Mosimane anapaswa kuwajibika kwa upangaji wake wa kikosiusimamizi wa mchezo na kipigo kutoka kwa Simba. Alifanya makosa katika ufanyaji wa mabadiliko na kuigharimu Al Ahly mbele ya Simba na alikosa ujasiri wa kushambulia katika mabadiliko ya mwisho," alisema Gomaa.

Bao pekee la mshambuliaji Luis Miquissone liliifanya Al Ahly ijikute ikiangukia nafasi ya tatu kwenye msimamo wa kundi A nyuma ya Simba inayoongoza, AS Vita iliyo katika nafasi ya pili wakati huo Al Merrikh ya Sudan ikishika mkia.

Kipigo hicho kutoka kwa Simba kilikuja siku chache baada ya Al Ahly kumaliza katika nafasi ya tatu kwenye mashindano ya Kombe la Dunia la Klabu yaliyofanyika Qatar.