Simba Ahly tiketi bado zipo

KUELEKEA mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Simba na Al Ahly, tiketi za mechi hiyo zimeonekana kuendelea kuuzwa kwenye maeneo mbali mbali ya jiji la Dar es Salaam.

Mitaa ya Magomeni, Sinza na Msimbazi Kariakoo ambapo ndipo makao makuu ya Simba wadau wa soka tofauti wameonekana wakiingia sehemu walipo mawakala wakuu za tiketi za mechi hiyo na kujipatia tiketi zao.

Hapo awali kabla ya jana saa 6:00 usiku tiketi hizo zilikuwa zikiuzwa kwa bei za Sh 3,000 mzunguko, Sh 15,000 VIP B na Sh 30,000 VIP lakini mpaka sasa zote zimepanda bei ambapo zile za mzunguko zinazoonekana kununuliwa kwa wingi kuuzwa Sh 5000.

Hilo halijawazuia wanasimba na wadau wengine wa soka kununua tiketi hilo kwani wamejazana kwa mawakala wakinunua tiketi bila kujali kupanda kwa bei.

Sambamba na hilo, gari dogo aina ya Hiace lililobandikwa logo za Simba na rangi nyekundu limeonekana mitaa ya Magomeni likiendelea kuuza tiketi kwa wadau wa soka.

Mchezo huo ni wa pili kwa Simba kwenye michuano hiyo kwa msimu huu na mchezo wa kwanza walicheza na AS Vita ugenini DR Congo na kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Kwa mara ya Mwisho Ahly na Simba kukutana ilikua Februari 2019 kwenye uwanja wa Taifa (Sasa Benjamin Mkapa) na Simba waliibuka na ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na Meddie Kagere.