Sevilla FC yathibitisha kuzivaa Simba, Yanga Uwanja Taifa

Muktasari:
Sevilla ina wachezaji 11 wanaocheza Timu za taifa kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Argentina, Hispania na Italia
Dar es Salaam. Sevilla FC imethibitisha kumalizia maandalizi ya msimu mpya wa ligi kwa kucheza na moja kati ya Simba au Yanga katika ziara yake nchini Tanzania.
Kampuni ya Michezo ya Kubashiri ya SportPesa kwa kushirikiana na La Liga imefanikisha ziara hiyo ya kuileta Sevilla nchini Tanzania kwa ajili ya ziara ya kimichezo inayokwenda kwa jina la ‘SportPesa Laliga Challenge’.
Mchezo huo umepangwa kupigwa Mei 23, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam ambao utakuwa sehemu ya maandalizi ya Sevilla kujiandaa na msimu mpya wa ligi.
“La Liga imepanga kuwa karibu na mashabiki wake, hivyo ni nafasi ya kipekee kwa kila shabiki Mtanzania wa Sevilla kupata nafasi ya kuiona,”alisema Oscar Mayo ambaye ni mratibu wa La Liga.
Mkuu wa Utawala na Udhibiti wa Kampuni ya SportPesa Tanzania, Tarimba Abass alisema shukrani kubwa kwa La Liga kwa kukubali kuja nchini katika ziara yao kufunga maandalizi ya msimu mpya wa ligi, wachezaji wetu watapata nafasi ya kuonyesha vipaji walivyokuwa navyo.
Katibu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wilfred Kidao alisema “siyo jambo ndogo kupata ugeni wa klabu kubwa kama Sevilla ambayo inashiriki ligi bora ya La Liga.
“Sevilla ina wachezaji 11 wanaocheza Timu za taifa kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Argentina, Hispania na Italia, hivyo kama TFF tunaahidi kushirikiana na SportPesa kuhakikisha maandalizi yote yanakwenda vizuri katika kuelekea mchezo huo.”