Ninja awajibu wanaombeza upigaji penati

BEKI wa Yanga Abdallah Shaibu 'Ninja' amesema hata kesho Jumatano kama itatokea wameingia kwenye mikwaju ya panalti watakapokutana na Simba katika fainali za Kombe la Mapinduzi yupo tayari kupiga panati.

Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Ninja kupiga penati tangu ajiunge Yanga ambapo amesema hakuwahi kupata nafasi hiyo ya kupiga penati.

Jana Jumatatu, Yanga walicheza mechi ya nusu fainali dhidi ya Azam FC ambapo walishinda kwa penalti 5-4 baada ya dakika 90 kumalizika kwa sare ya bap 1-1.

Katika penati hizo, Ninja alikuwa miongoni mwa wapigaji lakini mashabiki wengi waliofika kushuhudia mechi hiyo hawakuwa na imani yake ambapo walijua kuwa angekosa na Yanga kutolewa mashindanoni.

Akizungumza leo Jumanne Januari 12, 2021, Ninja amesema kuwa alifundishwa kupiga penati kabla ya mechi hiyo na kocha Cedric Kaze alimwambia ikitokea wameingia kwenye matatu basi yeye atapiga penati ya tano.

"Kwenye machi kama hizi lolote linaweza kutokea, mnaweza kushinda ndani ya dakika 90 ama nyongeza au kwa penati, hivyo wakati wa kujiandaa tulifundishwa namna ya kupiga penati na nilipangwa kupiga penati ya tano.

"Tulitaka kumaliza mechi ndani ya dakika 90 lakini haikuwa hivyo, tukaingia kwenye matuta ila nataka kuwaambia mashabiki kwamba wasikariri mpiga penati wanapaswa kumwamini kila mchezaji anayepewa jukumu hilo, hata ikitokea mechi ya fainali ikawa hivyo nitapiga nikipangwa," amesema Ninja

Penati za Yanga kwa waliopata zilifungwa na Tuisila Kisinda, Mukoko Tonombe, Paul Godfrey, Abdallah Shaibu na Zawadi Mauya wakati Michael Sarpong akikosa penati ya kwanza.

Upande wa Azam nyota wao wawili walikosa penati hizo ambao ni Awesu Awesu na Daniel Amour huku Bruce Kangwa, Ally Niyonzima, Mudathir Yahya na Wadada wakipata.