Namungo yazoa Simba, Yanga, Azam

Muktasari:
- Jangwani nako hawajabaki salama kwani nayo inajiandaa kupoteza wachezaji wake watatu, Pastory Ngonyani, Yohana Mkomola na Said Makapu, mbali na kiungo mshambuliaji wa zamani wa Simba anayekipiga African Lyon, Haruna Moshi ‘Boban’.
KAMA unaichukulia poa klabu ya Namungo inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza (FDL), basi pole yako kwani jamaa hawana utani hata kidogo.
Namungo ya mkoani Lindi inataka kucheza Ligi Kuu Bara msimu ujao na katika kuthibitisha hilo, imekomba nyota kadhaa kutoka ndani ya timu za Simba, Yanga na Azam ili kuimarisha kikosi chao kupitia dirisha dogo la usajili.
Namungo tayari imewanasa nyota wawili wa Azam, Mbaraka Yusuf na Oscar Masai ambao wapo hatua za mwisho za uhamisho huku ikielezwa rada zingine zimetua kwa washambuliaji wa Simba, Mohamed Rashid na Marcel Kaheza.
Jangwani nako hawajabaki salama kwani nayo inajiandaa kupoteza wachezaji wake watatu, Pastory Ngonyani, Yohana Mkomola na Said Makapu, mbali na kiungo mshambuliaji wa zamani wa Simba anayekipiga African Lyon, Haruna Moshi ‘Boban’.
Azam wameruhusu Mbaraka kwenda Namungo wakiamini ndio timu atakayopata nafasi ya kucheza, japo walipokea ofa nyingi za kumwomba kwa mkopo ikiwemo KMC, Prisons, Kagera Sugar na Arusha United sawa na Mo Rashid ambaye maombi mengi yametua mezani kwa Simba ambayo ni Prisons, KMC, Singida United na Mwadui.