Malimi asaka rekodi Mtibwa Sugar

Muktasari:
- Timu hiyo iliyoshuka Ligi Kuu Bara msimu uliopita, imeanza kibabe katika mechi 10 (kabla ya jana) ikishinda saba, sare mbili na kupoteza moja ikiwa na alama 23.
ACHANA na mechi ya jana dhidi ya Mbuni FC ugenini, lakini moto wa Mtibwa Sugar ni mkali kwenye Ligi ya Championship ikipambana kurejea Ligi Kuu Bara msimu ujao, huku takwimu zikimpa tabasamu kipa Costantine Malimi.
Timu hiyo iliyoshuka Ligi Kuu Bara msimu uliopita, imeanza kibabe katika mechi 10 (kabla ya jana) ikishinda saba, sare mbili na kupoteza moja ikiwa na alama 23.
Mtibwa Sugar ndiyo timu iliyoshinda mechi zote za nyumbani (tano), ikifunga mabao mengi (17).
Malimi aliyetua msimu huu akitokea Geita Gold, amedaka katika mechi 10 huku akiruhusu mabao matano pekee akiwa ndiye mwenye ‘cleen sheet’ nyingi mpaka sasa (saba).
Kipa huyo aliliambia Mwanaspoti kwamba siri ya ubora wake ni kusikiliza na kufuata maelekezo ya benchi la ufundi akilenga kuipambania timu hiyo irejee Ligi Kuu jambo ambalo atakuwa ameua ndege wawili kwa kuuza kipaji chake.
“Naangalia kwanza malengo ya timu kupambana iweze kurudi Ligi Kuu maana ikifanikiwa na mimi nakuwa nimefanikiwa. Nashukuru kwa kuaminiwa na kudaka mechi zote mpaka sasa,” alisema Malimi
Aliongeza kuwa, “matokeo tunayopata yanaleta motisha. Tunapofanya vizuri inanipa moyo nazidi kujituma na kuzidisha sehemu nilipoishia niendelee zaidi ya hapo.”